Rais Xi asisitiza kuimarisha ujenzi wa serikali mtandao na kuendeleza mageuzi ya usimamizi wa fedha

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 20, 2022

BEIJING - Rais Xi Jinping wa China Jumanne wiki hii amesisitiza juhudi za kuimarisha ujenzi wa serikali mtandao na kuendeleza mageuzi ya mfumo wa mambo ya utawala ya fedha katika ngazi ya mikoa na chini ya ngazi ya mikoa.

Xi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya Kijeshi ya China, ameyasema hayo alipokuwa akiongoza mkutano wa 25 wa Kamati Kuu ya Kuendeleza Mageuzi kwa kina na kwa pande zote.

Mkutano huo ulipitia na kupitisha miongozo kadhaa kuhusu masuala yaliyotajwa hapo juu, pamoja na miongozo mingine ya kuanzisha mfumo wa vigezo vya ukaguzi wa maofisa wanaomaliza muda wao juu ya usimamizi wa maliasili, na kuimarisha utaratibu wa motisha kwa watafiti wa kisayansi, ikiwa ni pamoja na mpango kazi wa kuboresha usaidizi wa kifedha kwa uvumbuzi.

Xi amesisitiza juhudi za kutekeleza kikamilifu mkakati wa kitaifa wa kuimarisha nguvu ya China katika mtandao wa intaneti, akihimiza matumizi mapana ya teknolojia ya kidijitali katika usimamizi na huduma za serikali.

“Uendeshaji wa serikali mtandao kwa akili bandia unapaswa kuhimizwa ili kutoa msaada thabiti kwa ajili ya mambo ya kisasa ya mfumo wa utawala wa nchi na uwezo wa usimamizi” Xi amesema.

Kuhusu mageuzi ya mfumo wa usimamizi wa fedha nchini humo, Xi ameeleza kuwa uhusiano wa usimamizi wa fedha kati ya serikali za ngazi ya mikoa na chini yake unapaswa kunyooshwa ili kuwezesha uwiano wa kimantiki kati ya mamlaka na uwajibikaji, mgawanyo wa mapato ulio sanifu zaidi, mgawanyo wa rasilimali za fedha wenye uwiano, na usalama imara wa mapato na matumizi katika ngazi ya msingi.

Xi Ametoa wito wa kuharakisha ujenzi wa soko la ndani lililounganishwa, kukuza usawa wa huduma za kimsingi za umma na kuendeleza maendeleo ya kiwango cha juu.

Kuhusu kuanzisha mfumo wa vigezo vya ukaguzi wa maofisa wanaomaliza muda wao juu ya usimamizi wa maliasili, Xi amesema mfumo huo lazima uwe wa kisayansi, sanifu na wenye ufanisi ili kuwahimiza maofisa kutimiza wajibu wao kuhusu usimamizi wa maliasili na ulinzi wa ikolojia.

Pia amehimiza kuzingatia viungo dhaifu katika huduma za kifedha kwa uvumbuzi wa kisayansi, na kuongeza usaidizi wa kifedha kwa uvumbuzi, ili kuhakikisha mfumo wa kifedha unakidhi mahitaji ya uvumbuzi wa kisayansi katika zama mpya.

Li Keqiang, Wang Huning na Han Zheng, ambao ni wajumbe wa kudumu wa Ofisi ya Siasa ya Kamati Kuu ya CPC na Manaibu wakuu wa kamati kuu ya kuendeleza mageuzi kwa kina na kwa pande zote, walihudhuria mkutano huo.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha