Rais Xi Jinping azungumza na Rais wa Cote d'Ivoire kwa njia ya simu

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Desemba 21, 2022

BEIJING - Rais wa China Xi Jinping Jumanne mchana alifanya mazungumzo kwa njia ya simu na Rais wa Cote d'Ivoire Alassane Ouattara kutokana na ombi la rais huyo.

Akiitaja Cote d'Ivoire kuwa mshirika muhimu wa ushirikiano wa China barani Afrika, Rais Xi amesema mwaka ujao itatimia miaka 40 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia wa nchi hizo mbili, jambo ambalo linastahili kuadhimishwa kwa pamoja.

Rais Xi amesema China inathamini sana ufuataji thabiti wa Cote d'Ivoire kwenye kanuni ya kuwepo kwa China moja, na iko tayari kuendelea kusaidiana katika masuala yanayohusu maslahi yao ya msingi, kuunganisha na kuimarisha uhusiano wa China na Cote d'Ivoire, na kusukuma mbele maendeleo ya uhusiano wa pande hizo mbili kwenye viwango vipya.

Huku akieleza kuwa ushirikiano kati ya China na Cote d'Ivoire una matarajio mapana, Rais Xi amesema kuwa China iko tayari kuimarisha ushirikiano na Cote d'Ivoire katika pande zote, kupanua biashara ya mazao ya kilimo, kuimarisha ushirikiano wa nchi hizo mbili katika kupanda mpunga na kakao, na kuunga mkono Cote d'Ivoire kupanua na kuimarisha sekta yake ya kakao. Ameeleza matumaini yake kuwa miradi husika inayoungwa mkono na kujengwa na upande wa China itakamilika haraka iwezekanavyo na kuanza kutumika.

Amesema China iko tayari kuendelea kuhimiza makampuni ya China kuwekeza na kufanya biashara nchini Cote d'Ivoire, na kupanua ushirikiano wa pande mbili katika sekta kama vile uchumi wa kidijitali na nishati mpya.

Pamoja na kusema China inapenda kushirikiana na Cote d'Ivoire na nchi nyingine za Afrika ili kudumisha haki na usawa wa kimataifa pamoja na maslahi ya pamoja ya nchi zinazoendelea, Rais Xi amesema, China iko tayari kuendelea kutekeleza kwa vitendo Pendekezo la Maendeleo ya Dunia na mipango kazi ya Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) ili kuhimiza maendeleo ya Afrika.

Kwa upande wake, Ouattara amempongeza tena Rais Xi kwa kuchaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China, akisema kwamba alifurahishwa sana na ziara yake ya kiserikali nchini China Mwaka 2018 na anatarajia sana maadhimisho ya miaka 40 ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Huku akisema Cote d'Ivoire ina hisia za kirafiki kwa watu wa China, Ouattara amesema nchi yake inafuata kwa uthabiti kanuni ya kuwepo kwa China moja na inaunga mkono kikamilifu Pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja na FOCAC.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha