Uchumi wa Mbio za Marathon warejea tena China

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 18, 2023

Tarehe 16,Aprili, mashindano ya mbio za marathon yalianza katika maeneo mengi nchini China kama vile Beijing, Shanghai na Wuhan, mashindano karibu 30 yalifanyika katika wikiendi iliyopita yaani tarehe 15 na 16. Wakati miji kadhaa inapotangaza kurejesha mashindano ya mbio za marathon, uchumi wa marathon nao unarejea pia.

Pilikapilika za Mbio za Marathon

Mashindano ya mbio za marathon yamekuwa yakifanyika kwa kishindo maeneo mbalimbali kote nchini China. “Ripoti ya kazi ya Mbio za Barabarani ya Shirikisho la Riadha la China 2023" inaonyesha kuwa katika nusu ya kwanza ya mwaka huu, mashindano ya mbio za barabarani 133 tayari yamesajiliwa. Duniani kote, Shirikisho la Riadha la Dunia limetangaza kuwa mashindano ya mbio za marathon ya 2023 yaliyoidhinishwa yamefikia 238. Miongoni mwao, kuna mashindano 67 nchini China, ikishika nafasi ya kwanza duniani.

Nguvu nzuri ya kuchochea ukuaji wa uchumi

Kwa mujibu wa Guo Bin, naibu katibu mkuu wa Kituo cha Utafiti wa Sekta ya Michezo ya Kitaifa cha Chuo Kikuu cha Peking, ongezeko la mashindano ya mbio za marathoni la hivi karibuni siyo tu limechangamsha shughuli za sasa za ufanisi wa mashindano na soko la matumizi katika manunuzi ya bidhaa za michezo, lakini pia limeleta vichocheo vipya vya ukuaji wa uchumi, na kuchochea maendeleo ya tasnia na nyanja nyingine.

Ripoti inaonyesha kuwa Mwaka 2020, wakimbiaji wa China walitumia wastani wa zaidi ya Yuani 11,000 kwa kila mtu, ikiwa ni pamoja na ununuzi wa mahitaji ya kila siku vikiwemo vifaa vya mazoezi, mavazi na vyakula vya lishe na gharama nyinginezo. Asilimia 50 ya wakimbiaji wamekuwa na uzoefu wa kwenda maeneo mengine kushiriki kwenye mashindano. Asilimia 71 ya wakimbiaji wanaoshiriki kwenye mashindano huonja vyakula vya kienyeji, na 64% hufanya matembezi ya kitalii pale.

Ushindani mkali masokoni

Mashindano ya mbio za marathon pia ni moja wapo ya mambo muhimu ya kutangaza bidhaa za michezo za chapa kuu.

Takwimu zinaonyesha kuwa Chapa ya Vifaa vya Michezo ya Xtep imefadhili mashindano ya mbio za marathon zaidi ya 1,000 tangu kufadhili mbio za marathon za kwanza Mwaka 2007. 

Mbali na chapa za michezo, mashindano ya mbio za marathon pia yamevutia ushiriki wa kampuni nyingi za chakula na vinywaji.

Taasisi za kifedha pia zinaunga mkono kwa nguvu shughuli zinazohusiana na mbio za marathon. Inafahamika kuwa Mfuko wa Huaxia ulifadhili Mbio za Nusu Marathon za Beijing, Benki ya Maendeleo ya Shanghai Pudong ilifadhili Mbio za Nusu Marathon za Shanghai, na mbio za Marathon za Wuhan 2023 zilifadhiliwa na Benki ya China.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha