Rais Xi Jinping atuma barua ya pongezi kwa Baraza la Zhongguancun

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 26, 2023

BEIJING - Rais wa China Xi Jinping ametuma barua ya pongezi kwa Baraza la Zhongguancun la Mwaka 2023 ambalo limefunguliwa Alhamisi hapa Beijing.

Rais Xi amesema, wakati raundi mpya ya mapinduzi ya kisayansi na mageuzi ya kiviwanda yakiendelea kubadilika, binadamu wanahitaji ushirikiano, uwazi na uchangiaji zaidi wa kimataifa kuliko wakati mwingine wowote ili kushughulikia matatizo ya pamoja ya maendeleo.

“Ikiwa imejitolea kwa mkakati wenye manufaa ya pande zote wa kufungua mlango, China iko tayari kuungana na nchi nyingine kuhimiza uvumbuzi wa teknolojia za kisayansi na kuifanya sayansi na teknolojia kuwahudumia watu wa nchi zote vizuri zaidi,” amesema Rais Xi.

Amesisitiza kuwa Beijing inapaswa kutumia kikamilifu nguvu zake katika elimu, sayansi, teknolojia na vipaji, kuratibu uvumbuzi wa kisayansi na kitaasisi, kuendelea kuhimiza mageuzi ya miradi ya majaribio katika eneo la Zhongguancun, kuharakisha zaidi ujenzi wa eneo maalum la sayansi na teknolojia linaloongoza duniani, na kufanya bidii za kuwa kinara katika uvumbuzi wa teknolojia za kisasa na maendeleo ya viwanda vinavyotumia teknolojia ya hali ya juu na vya kisasa.

Likiwa na kaulimbiu ya "Ushirikiano Wazi kwa Mustakabali wa Pamoja wa Baadaye," Baraza la Zhongguancun la Mwaka 2023 linaandaliwa kwa pamoja na Wizara ya Sayansi na Teknolojia ya China, Kamati ya Kitaifa ya Maendeleo na Mageuzi ya China, Wizara ya Viwanda na Teknolojia ya Habari ya China, Kamati ya Usimamizi na Uendeshaji wa Mali za Viwanda vya Kiserikali ya Baraza la Serikali la China, Taasisi Kuu ya Sayansi ya China, Taasisi Kuu ya Uhandisi ya China, Shirikisho la Sayansi na Teknolojia la China, na serikali ya mji wa Beijing. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha