Kituo cha malipo ya kuvuka mpaka kwa kutumia fedha ya China, Yuan kati ya China na Afrika chafunguliwa Yiwu, China

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 30, 2023

Mandhari ya angani ya Soko la Biashara la Kimataifa la Yiwu huko Yiwu, Mkoa wa Zhejiang, Mashariki mwa China (Picha: VCG)

Mandhari ya angani ya Soko la Biashara la Kimataifa la Yiwu huko Yiwu, Mkoa wa Zhejiang, Mashariki mwa China (Picha: VCG)

Kituo cha malipo ya kuvuka mpaka kwa kutumia fedha ya China, Yuan kati ya China na Afrika kimefunguliwa huko Yiwu, China, mji ambao ni soko kubwa la mauzo kwa jumla ya bidhaa ndogo duniani, katika Mkoa wa Zhejiang, Mashariki mwa China, kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa kwenye ukurasa wa Yiwufabu, ukurasa rasmi ya Mtandao wa WeChat wa serikali ya Mji wa Yiwu siku ya Jumatatu.

Hatua hiyo inatazamiwa kutoa huduma za malipo na kuidhinisha mizigo ya bidhaa kwa njia mbalimbali kwa kampuni za biashara za China na Afrika, kupunguza gharama na hatari za ubadilishaji wao wa fedha na kukuza biashara kati ya China na Afrika, wamesema wataalam na wafanyabiashara.

Kwa mujibu wa serikali ya Yiwu, kituo hicho kitapanua shughuli za malipo ya kuvuka mipaka kwa kutumia Yuan barani Afrika, kuimarisha ushirikiano na matawi ya benki za China na taasisi za fedha barani Afrika, kuanzisha njia za malipo ya kuvuka mipaka kwa kutumia Yuan na kutafuta namna ya uhamishaji wa mali wa kuvuka mipaka na ununuzi na mauzo kati ya benki.

Kuanzishwa kwa kituo hicho kunatoa njia rahisi zaidi ya suluhu kwa mabadilishano ya kiuchumi na kibiashara kati ya Yiwu na Afrika, huku baadhi ya wafanyabiashara wakitarajia kuwa malipo hayo ya kuvuka mipaka kwa kutumia Yuan yatapunguza gharama na hatari za viwango vya ubadilishaji fedha huku kukiwa na hali tata na tete ya kimataifa.

Liu Hongwu, mkuu wa masomo ya Afrika katika Chuo Kikuu cha ualimu cha Zhejiang kilichoko mashariki mwa China, amesema kuwa ukosefu wa dola ndilo suala kubwa zaidi ambalo limekuwa likizuia biashara inayokuwa kwa kasi kati ya China na Afrika katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.

"Kwa vile biashara kati ya China na Afrika ina msingi mkubwa na imara katika bidhaa na huduma, ushirikiano katika uwezo wa uzalishaji na maendeleo ya viwanda, watu sasa wanatambua uwezekano wa washirika hao wawili wa kibiashara kuiondoa dola katika mchakato wa biashara ya nje," Liu amesema.

Afrika ni mshirika mkubwa zaidi wa kibiashara wa Mji wa Yiwu, na kuna wafanyabiashara Waafrika karibu 2,000 wanaoishi katika mji huo. Mwaka 2022, thamani ya jumla ya biashara ya Yiwu na Afrika ilifikia yuan bilioni 84.02 (sawa na karibu dola bilioni 11.87), ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.2.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha