Viongozi na Wataalam kutoka Afrika wasifu hotuba ya Rais Xi kwenye ufunguzi wa Baraza la Tatu la Ushirikiano wa Kimataifa wa Ukanda Mmoja, Njia Moja

By Aris (Tovuti ya Gazeti la Umma) Oktoba 19, 2023

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu nchini Tanzania, Yahaya Nawanda (kushoto) akiwa katika mahojiano na mwandishi wa habari wa People’s Daily Online, Aris. (People’s Daily)

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu nchini Tanzania, Yahaya Nawanda (kushoto) akiwa katika mahojiano na mwandishi wa habari wa People’s Daily Online, Aris. (People’s Daily)

Viongozi na wataalam kutoka Afrika wamesifu na kupongeza hotuba ya Rais Xi Jinping wa China aliyoitoa kwenye ufunguzi wa Mkutano wa Viongozi wa Baraza la Tatu la Ushirikiano wa Kimataifa wa Ukanda Mmoja, Njia Moja ambapo wamesema imejaa ujumuishi na kuingiza mapendekezo mapya katika ustawi wa pamoja.

Katika hotuba yake ya ufunguzi siku ya Jumatano Rais Xi ametanagza hatua nane za kujenga kwa kiwango cha juu Pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja ikiwa ni pamoja na muunganisho wa pande nyingi wa Ukanda Mmoja, Njia Moja, kuunga mkono uchumi wa Dunia ulio wazi, kufanya ushirikiano wa kivitendo wa BRI, msisitizo katika uchumi wa kidijitali na ubunifu wa teknolojia mpya.

Akizungumzia hotuba hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu nchini Tanzania Yahaya Nawanda ambaye amehudhuria ufunguzi huo kwa mwaliko wa Rais Xi mwenyewe, amesema mambo manane ambayo Rais Xi ameyapendekeza yanaenda sambamba na mipango ya Serikali ya Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar Hussein Mwinyi.

Amesema maeneo kama uchumi wa buluu, uhamishaji wa teknolojia na uchumi wa kidijitali yamekuwa yakitiliwa mkazo na serikali ya Tanzania na kwamba hotuba hiyo ya Rais Xi na pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja vinaendana na mipango ya Serikali ya Tanzania.

Walter Nyamukondiwa, Mkuu wa Habari na Masuala ya Mapya yanayofuatiliwa wa Gazeti la The Herald nchini Zimbabwe amesema hotuba hiyo ilikuwa jumuishi, na moja ya masuala muhimu aliyosisitiza ni maendeleo jumuishi, kwamba, washirika na wadau katika BRI waende pamoja kama kitu kimoja katika uanuai wao lakini lengo likiwa ni kuleta maendeleo kwa kila mmoja wa washiriki.

“Katika nchi nyingi zinazoendelea kuna upungufu wa miundombinu na suala moja muhimu ambalo BRI inashughulikia ni hili. Katika hotuba yake kulikuwa na uamuzi wa makusudi wa kuleta kila mtu kwenye mwelekeo sahihi katika suala la maendeleo ya miundombinu” amesema.

Amesema, suala lingine alilosisitiza ni uhamishaji wa teknolojia, huku akieleza kuwa kwa mtazamo wa nchi zinazoendelea kipengele hiki muhimu kwa maendeleo kinakosekana. “Nadhani ni muhimu kulijumuisha hili kwenye ajenda ya BRI” amesema.

Kwa upande wake mwandishi wa habari za kisiasa wa gazeti la Star la Kenya, Moses Odhiambo amesema hotuba ya Rais Xi imesisitiza haja ya Dunia kuja pamoja na kuzungumza kwa sauti moja katika masuala ya msingi ambayo yanaathiri kila mmoja, kwani nchi zinahitajiana na mahitaji yanafanana ingawa huzidiana kiasi tu.

Kuhusu uchumi wa kidijitali suala ambalo Rais Xi amelitaja katika hatua nane za utekelezaji za BRI, Odhiambo amesema, ni suala ambalo tayari lipo nasi na linaendelea kuwa kubwa. Amesema Afrika inaonekana bado kuwa nyuma, inahitaji kuweka jitihada kubwa hasa katika biashara ya mtandaoni, miamala ya kidijitali na kutunga kanuni za uratibu na usimamizi wa teknolojia mpya hususan zile za akili bandia.

Naye Abubakar Harith ambaye ni mwandishi wa habari na mtangazaji wa Shirika la Habari la Zanzibar nchini Tanzania amesema, hotuba ya Rais Xi imetaja mambo muhimu manane ambayo kwa Afrika yote yanafaa na nchi za Afrika zinahitaji kuweka mazingira wezeshi ya kuwa sehemu yake.

Amesema katika mambo yote hayo manane, eneo la uchumi wa kidigitali na matumizi ya kiteknolojia Afrika bado inatumia kwa tija ndogo ikilinganishwa na nchi nyingine hasa zilizoendelea. Amesema, hotuba ya Rais Xi katika kutilia maanani maeneo haya ni muafaka ingawa uharaka, utayari, mazingira rafiki na utekelezaji wake unahitaji Afrika yenyewe kuwa tayari.

Waandishi wa habari kutoka Afrika, Moses Odhiambo wa gazeti la Star la Kenya (kushoto), Abubakar Harith, mtangazaji wa Shirika la Habari la Zanzibar nchini Tanzania (kati) na Francis Mtalaki wa Mombasa, Kenya wakiwa katika picha ya pamoja. (People’s Daily Online)

Waandishi wa habari kutoka Afrika, Moses Odhiambo wa gazeti la Star la Kenya (kushoto), Abubakar Harith, mtangazaji wa Shirika la Habari la Zanzibar nchini Tanzania (kati) na Francis Mtalaki wa Mombasa, Kenya wakiwa katika picha ya pamoja. (People’s Daily Online)

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha