Meli yalipuka mjini Mombasa, Kenya

(CRI Online) Desemba 28, 2023

Mtu mmoja amejeruhiwa katika mlipuko uliotokea ndani ya meli ya mafuta iliyokuwa imetia nanga karibu na kituo cha meli cha African Marine kilichoko Liwatoni, Likoni, mjini Mombasa, Kenya.

Akithibitisha tukio hilo, Mkuu wa Polisi wa kituo cha Kati, Bw. Maxwel Agoro, amesema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa mlipuko huo umesababishwa na mrundikano wa gesi ndani ya matangi ya kusafirisha mafuta yaliyokuwa ndani ya meli hiyo.

Mlipuko huo mkubwa ulitetemesha majengo yaliyokuwa umbali wa kilomita mbili kutoka kwenye eneo la tukio, na kusababisha moto ulioteketeza sehemu za meli hiyo.

Hata hivyo, hatua za haraka zilizochukuliwa na Mamlaka ya Bandari Kenya (KPA) kwa kupeleka maboti na magari ya zimamoto zilizuia madhara zaidi.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha