Rais Xi Jinping ajibu barua kutoka kwa wajumbe wa wanafunzi na wahitimu Wakenya wa Chuo Kikuu cha Beijing Jiaotong

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Januari 24, 2024

BEIJING - Rais wa China Xi Jinping amejibu barua kutoka kwa wajumbe wa wanafunzi na wahitimu Wakenya wa Chuo Kikuu cha Beijing Jiaotong, akiwahimiza kuendelea kuchangia katika urafiki kati ya China na Kenya na China na Afrika.

Katika majibu yake hayo ya Januari 17, Rais Xi ameeleza kuwa China na Kenya zinafurahia urafiki wa muda mrefu uliotukuka na kwamba Pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja limebadilisha matumaini ya maendeleo na ustawishaji wa China na Kenya kuwa hali halisi, na kuunganisha kwa karibu ustawi wa watu wa nchi hizo. Amesema, Reli ya Mombasa-Nairobi ni mradi kinara na mfano mzuri wa ushirikiano wa Ukanda Mmoja, Njia Moja wa China na Kenya.

"Nimefurahi kuona kwamba mmeungana na China kupitia barabara hii ya kuelekea furaha. Mmeshuhudia na kunufaika na urafiki na ushirikiano kati ya China na Kenya na China na Afrika, na mmesaidia kujenga na kueneza urafiki na ushirikiano kati ya China na Kenya na China na Afrika," Rais Xi amesema.

Tukitazama mbele, picha nzuri ya Ukanda Mmoja, Njia Moja na dira kuu ya uhusiano wa wenzi wa ushirikiano wa kimkakati wa pande mbili za China na Kenya zinahitaji vijana wengi wenye uwezo na ari kubwa katika kuzifikia, amesisitiza Rais Xi.

"Inatarajiwa kwamba mtaweza kujifunza ujuzi wa kitaaluma vizuri, kuendeleza urafiki wa jadi, kujitolea kwa nguvu kwenye ushirikiano wa pande mbili, kuelezea simulizi nzuri za urafiki wa China na Afrika, na kutoa mchango mkubwa kwa ajili ya ujenzi wa jumuiya ya kiwango cha juu ya China na Afrika yenye mustakabali wa pamoja," Rais Xi amesema.

Hivi majuzi, wajumbe wa wanafunzi na wahitimu Wakenya wa Chuo Kikuu cha Beijing Jiaotong walimwandikia barua Rais Xi, wakielezea furaha yao kubwa ya kuja China kusoma na kupata ujuzi wa uendeshaji na usimamizi wa reli. Pia walieleza matumaini yao ya kuwa daraja la urafiki kati ya Kenya na China na kuchangia katika kuimarisha urafiki na ushirikiano kati ya nchi hizo mbili na kujenga jumuiya ya binadamu yenye mustakabali wa pamoja. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha