Maonyesho ya biashara ya China na Afrika nchini Kenya yamalizika kwa wito wa kuwa na uhusiano thabiti wa kibiashara

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 13, 2024

NAIROBI - Maonesho ya Uchumi na Biashara ya China na Afrika (CAETE) barani Afrika (Kenya) 2024 yamemalizika siku ya Jumamosi huko Nairobi, mji mkuu wa Kenya, huku washiriki wakisisitiza wito wa kuimarisha uhusiano wa kibiashara kati ya China na Afrika.

Pius Rotich, meneja mkuu wa uhimizaji wa uwekezaji na maendeleo ya biashara katika Idara ya Uwekezaji ya Kenya, amesema kuwa maonyesho hayo yametoa jukwaa kwa kampuni za China kuanzisha uhusiano na wenzao kutoka kote barani Afrika.

"Tunatumai kuwa uhusiano ulioanzishwa katika maonyesho hayo unataongeza biashara kati ya China na Afrika," Rotich amesema.

Maonyesho hayo ya siku tatu ambayo yalivutia ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Mkoa wa Hunan wa katikati ya China yameandaliwa na sekretarieti ya Kamati Maandalizi ya Maonesho ya Uchumi na Biashara ya China na Afrika (CAETE) pamoja na Wizara ya Uwekezaji, Biashara na Viwanda ya Kenya.

Gao Wei, mkurugenzi mkuu wa Afripeak Expo Kenya ambaye alikuwa mmoja wa waandaaji wa maonyesho hayo, amesema kuwa maonyesho hayo yameleta mvuto mkubwa kwa wafanyabiashara wa Afrika ambao walikuwa na shauku ya kuanzisha uhusiano na kampuni za China.

Kwenye maonyesho hayo, angalau makubaliano kumi ya kibiashara yametiwa saini kati ya kampuni za Afrika na za China yakiwemo makubaliano kuhusu mradi wa Kiwanda cha utengenezaji wa mafuta ya Alizeti nchini Tanzania, Mradi wa Ujenzi wa Ghala la Umma la Ng’ambo wa Kundi la Kampuni za Bandari ya Nchi Kavu la Yongzhou na Djibouti pamoja na mradi wa ushirikiano katika biashara ya samaki wa kavu ya Kenya.

Maonyesho hayo yameonesha umaalumu wake wa kufanya makongamano, mawasiliano na kuanzisha uhusiano baina ya wafanyabiashara, na kuonesha bidhaa za kampuni zaidi ya 100 za vifaa vya mashine, chakula na mazao ya kilimo, vyombo vya kielektroniki na upashanaji habari, dawa na usambazaji bidhaa. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha