Ujumbe wa AU na IGAD wawasili Sudan Kusini kwa ajili ya upatanishi

(CRI Online) Mei 06, 2025

Ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Umoja wa Afrika (AU) na Mamlaka ya Kiserikali kuhusu Maendeleo ya Nchi za Afrika Mashariki (IGAD) umewasili nchini Sudan Kusini, ili kuendeleza mazungumzo ya amani kati ya serikali ya mpito ya umoja na upinzani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya nje ya nchi hiyo, ujumbe huo unaoongozwa na Mwenyekiti wa Kamisheni ya AU Mahmoud Ali Youssouf na Naibu Katibu Mtendaji wa IGAD Mohamed Abdi Ware, unatarajiwa kukutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Sudan Kusini Monday Semaya Kumba.

Ujumbe huo pia umepangwa kukutana na mshauri mwandamizi wa Rais Salva Kiir, Kuol Manyang Juuk, kabla ya kukutana na rais mwenyewe.

Hata hivyo, bado haijafahamika kama ujumbe huo utakutana na kiongozi wa upinzani Riek Machar, ambaye amewekwa kwenye kizuizi cha nyumbani tangu mwezi Machi.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha