Lugha Nyingine
Mradi wa maji unaoungwa mkono na China wapunguza kesi za kichocho nchini Tanzania

Wakazi wenyeji wakichukua maji safi kwenye bomba la umma lililowekwa chini ya mradi wa maji safi unaosaidiwa na China huko Chaani, Zanzibar, Tanzania, Machi 22, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)
ZANZIBAR - Shukrani na matumaini sasa ni sehemu ya maisha ya kila siku kwa Juma Makame Mohamed na Huzaima Bakari Haji, wakazi wawili wa Chaani ambao jamii yao imebadilishwa na mradi wa maji safi unaoungwa mkono na China.
"Tunashukuru kwa kuwasili kwa mradi huu wa Wachina katika jamii yetu," amesema Mohamed mwenye umri wa miaka 38.
Kwa miaka mingi, jamii hiyo ya Chaani ilitegemea mito na mifumo ya maji isiyoaminika. Wakati vyanzo vya maji kutoka Mamlaka ya Maji ya Zanzibar vilipokauka, wakati mwingine kwa siku nyingi, wakazi hawakuwa na chaguo ila kuchota maji kutoka vyanzo visivyo salama.
"Maji hayo hayakuwa salama. Watoto na watu wazima walikuwa katika hatari," Mohamed amekumbushia.
Leo, kwa kuzungusha bomba, maji safi yanatiririka kwa kasi, shukrani kwa mpango unaosaidiwa na China uliotekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la Afya Duniani na serikali ya Zanzibar.
Mabadiliko yamekuwa makubwa. Wakazi zaidi ya 250 katika jamii hiyo ya Chaani sasa wanapata maji salama, badala ya kutegemea mito iliyochafuliwa ambayo hapo awali ilikuwa chanzo kikuu cha maambukizi.
"Kichocho kimepungua kwa kiasi kikubwa," Mohamed amesema. "Watoto sasa wana afya njema zaidi kwa sababu hatuogi tena mtoni."
Kichocho, ugonjwa wa vimelea unaohusishwa na maji freshi yaliyochafuliwa, umekuwa kwa muda mrefu ukiathiri jamii za vijijini kote Zanzibar. Katika jamii hiyo ya Chaani, kingo za mito zilizokuwa zikijaa watu hapo awali zilikuwa vitovu vya shughuli za kila siku, na kuongeza hatari ya kupata ugonjwa huo.
"Kabla ya mradi huo, tulilazimika kuchota maji kutoka mito, hata wakati ilipokuwa michafu baada ya mvua," amesema Huzaima Bakari Haji mwenye umri wa miaka 27. "Watoto mara nyingi waliteseka kutokana na maumivu ya tumbo na magonjwa."
Sasa, maji safi yanapatikana ndani ya jamii ya Chaani.
Matokeo mazuri ya mradi huo yanaenea zaidi ya afya, kwani upatikanaji bora wa maji umeokoa muda kwa ajili ya shughuli za kiuchumi na majukumu ya nyumbani.
"Hapo awali, ilibidi utumie saa nyingi kuchota maji," Mohamed amesema. "Sasa unaenda kwenye bomba na kuendelea na siku yako."
Kwa mujibu wa Rashid Saleh Khamis, naibu meneja wa mpango wa magonjwa ya kitropiki yasiyopewa kipaumbele visiwani Zanzibar, mafanikio yanatokana na ushirikiano wa karibu na wataalamu wa China. "Tunafanya kazi kwa karibu na wenzetu Wachina kudhibiti na pengine kutokomeza kichocho," amesema.
Kwa Wang Wei, kiongozi wa timu ya wataalamu wa China, miundombinu ya maji ina jukumu muhimu katika kuvunja mzunguko wa magonjwa. "Tulijenga minara mitatu ya maji yenye vituo 24 vya usambazaji kwa jumla," amesema. "Hii inahakikisha upatikanaji wa maji safi wakati huohuo ikipunguza magonjwa yanayosababishwa na vimelea vya majini."
Mradi huu ni sehemu ya juhudi pana za ushirikiano wa afya kati ya China na Afrika zilizoanza mwaka 2016, zikichanganya uzoefu wa China katika kudhibiti magonjwa na utekelezaji wa ndani na uungaji mkono wa kimataifa.

Mnara wa maji uliojengwa chini ya mradi wa maji safi unaosaidiwa na China ukionekana Chaani, Zanzibar, Tanzania, Machi 22, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)

Mtoto akinywa maji kutoka kwenye bomba lililowekwa chini ya mradi wa maji safi unaosaidiwa na China huko Chaani, Zanzibar, Tanzania, Machi 22, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



