Lugha Nyingine
Kusanyiko kubwa la wanawake mjini Luanda laangazia uwezeshaji na masuala ya kijamii
LUANDA - Wanawake zaidi ya 100,000 walikusanyika Jumamosi katika Ghuba ya Luanda nchini Angola kuhudhuria Mkutano wa kwanza wa Wanawake wa Jimbo la Luanda, uliofanyika chini ya kaulimbiu ya “Wanawake wa Luanda, Kiini Kinacholeta Mageuzi."
Uliandaliwa na serikali ya jimbo hilo kama sehemu ya maadhimisho ya Mwezi wa Wanawake, tukio hilo liliwakutanisha washiriki kutoka manispaa zote 16 za jimbo hilo, likionyesha uanuwai wa wanawake wa Angola kwa kuzingatia makundi ya umri, asili ya kijamii, imani za kidini na misimamo ya kisiasa.
Akihutubia mkutano huo, Mkuu wa Jimbo la Luanda Luis Manuel da Fonseca Nunes alieleza wasiwasi juu ya kuongezeka kwa tabia potofu miongoni mwa baadhi ya vijana, akihimiza hatua za pamoja kutoka kwa taasisi za umma na jamii. Ametoa wito wa kuimarishwa kwa sera zinazolenga kinga, elimu, utoaji wa haki kwa wakati, na utekelezaji madhubuti wa adhabu.
Nunes pia amesisitiza hitaji la kujenga imani katika taasisi za serikali, akisema hakuna mwanamke anayepaswa kuhisi kutolindwa anapokabiliwa na ukatili au unyanyasaji, wala hakuna familia inayopaswa kubaki katika hali ya hatari kutokana na changamoto za kijamii.
Tukio hilo lilijumuisha mijadala kuhusu uwezeshaji wanawake, usawa wa kijinsia, na jukumu la wanawake katika maendeleo ya kitaifa, pamoja na shughuli za kitamaduni na burudani. Washiriki walishiriki uzoefu wao na kusisitiza umuhimu wa kuwatambua wanawake kuwa nguzo muhimu za maendeleo ya kijamii, kiuchumi, na kisiasa.
Maafisa wametoa wito kwa sekta zote za jamii kuimarisha juhudi za kulinda wanawake na kukuza ustawi wao, wakibainisha kuwa kulinda wanawake ni muhimu kwa kulinda familia na kuhakikisha mustakabali wa jamii.
Serikali ya Jimbo la Luanda imesisitiza dhamira yake ya kusukuma mbele sera zinazohimiza fursa sawa na kuimarisha nafasi ya wanawake kama nguzo ya maendeleo endelevu nchini Angola.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



