Benki ya Dunia yaeleza janga la UVIKO-19 limeleta "mabadiliko mabaya" katika maendeleo Duniani (2)

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Oktoba 14, 2021
Benki ya Dunia yaeleza janga la UVIKO-19 limeleta

WASHINGTON - Mkurugenzi wa Benki ya Dunia David Malpass amesema Jumatano ya wiki hii kwamba janga la UVIKO-19 linaendelea kuongeza umaskini na kiwango cha madeni katika nchi zenye kipato cha chini, ikionesha "mabadiliko mabaya" katika maendeleo.

"Tayari limesababisha karibu watu milioni 100 kuwa na umaskini uliokithiri. Hiyo ndiyo idadi inayoongezwa katika umasikini uliokithiri," Malpass amesema katika mkutano na waandishi wa habari wakati wa Mikutano ya Mwaka ya IMF na Benki ya Dunia.

"Tunashuhudia mabadiliko mabaya katika maendeleo. Mafanikio yaliyopatikana katika kupunguza umasikini uliokithiri yamerudishwa nyuma kwa miaka hata kwa muongo " aliendelea.

Akisisitiza kwamba ukosefu wa usawa unazidi kuongezeka kati ya nchi mbalimbali, Malpass amesema, kipato cha kila mtu katika nchi zilizoendelea kinaongezeka kwa asilimia 5 ikilinganishwa na asilimia 0.5 tu katika nchi zenye kipato cha chini mwaka 2021.

"Hali ya uchumi inabaki kuwa mbaya kwa nchi nyingi zinazoendelea. Kuna mfumuko mkubwa wa bei, fursa chache sana za ajira, kuna uhaba wa chakula, maji, na umeme," amesema, huku akitolea mfano wa kufungwa kwa viwanda na bandari na mkwamo katika mnyororo wa usafirishaji na usambazaji wa bidhaa.

Malpass pia alisisitiza kuwa nchi nyingi, hasa zile zilizoko nyumba kimaendeleo, zinakabiliwa na changamoto ya madeni. Katika Takwimu za Deni za Kimataifa zilizotolewa Jumatatu ya wiki hii, Benki ya Dunia imekadiria kuwa madeni ya nchi zenye kipato cha chini yameongezeka kwa asilimia 12 kufikia dola za kimarekani bilioni 860 mwaka 2020.

Huku akisisitiza kuwa nchi nyingi zinakabiliwa na msukosuko wamadeni ya nje au hatari kubwa, Malpass amewaambia waandishi wa habari kuwa "tunahitaji mpango kabambe, ikiwa ni pamoja na upunguzaji wa madeni, makubaliano mapya na uwazi zaidi ya madeni ili kupiga hatua katika changamoto hii."

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Renato Lu)

Picha