Kamati Teule ya Bunge la Marekani ya ghasia za Januari 6 kuwahoji maafisa zaidi wa serikali ya Trump (2)

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Novemba 10, 2021
Kamati Teule ya Bunge la Marekani ya ghasia za Januari 6 kuwahoji maafisa zaidi wa serikali ya Trump
Aliyekuwa Mshauri wa Usalama wa Kitaifa wa Marekani Michael Flynn akiondoka katika Mahakama Kuu kufuatia kusikilizwa kwa ombi lake mjini Washington D.C., Marekani, Desemba 1, 2017. (Xinhua/Ting Shen)

WASHINGTON, Marekani - Kamati Teule ya Bunge la Marekani inayochunguza ghasia za Januari 6 imeita maafisa 10 wa zamani katika serikali ya Rais wa 45 Donald Trump kufika mbele ya kamati hiyo, huku siku hiyo pia ofisi ya serikali ya uchunguzi na mashitaka ikitoa ripoti inayosema maafisa 13 walifanya kampeni za uchaguzi za Trump kinyume cha sheria na taratibu.

Kwa mujibu wa taarifa ya kamati teule hiyo iliyotolewa Jumanne ya wiki hii, viongozi wa zamani wanaoitwa ni pamoja na aliyekuwa Msemaji wa Ikulu ya Marekani Kayleigh McEnany, Mshauri Mkuu wa zamani wa Rais Stephen Miller, Mkurugenzi wa Utumishi wa Ikulu ya Marekani John McEntee, Naibu Mkuu wa zamani wa Jeshi Christopher Liddell, na mshauri wa usalama wa kitaifa wa Makamu wa Rais Mike Pence, Keith Kellogg.

Wengine walioitwa ni pamoja na Nicholas Luna, ambaye aliwahi kuwa msaidizi wa kibinafsi wa Trump; Cassidy Hutchinson, ambaye alikuwa msaidizi maalum wa rais wa zamani kwa masuala ya sheria; Kenneth Klukowski, aliyekuwa Wakili Mwandamizi Msaidizi wa Mwendesha Mashitaka Mkuu Jeffrey Clark; Benjamin Williamson, ambaye aliwahi kuwa mshauri Mkuu wa Ikulu ya White House Mark Meadows; na Molly Michael, ambaye aliwahi kuwa mratibu wa shughuli za Ofisi Kuu ya Ikulu ya Marekani.

"Akiwa msemaji wa Ikulu ya Marekani ulitoa taarifa nyingi kwa umma kutoka Ikulu ya Marekani na kwingineko kuhusu udanganyifu uliodaiwa katika uchaguzi wa Novemba 2020, ambazo watu walioshambulia Bunge la Marekani waliziunga mkono Januari 6" Kamati teule imeandika katika mwito wa Msemaji huyo wa zamani wa Ikulu McEnany.

Wito kwa Miller unadai kuwa yeye na wengine wa timu yake "walitayarisha maneno ya Rais Trump kwa mkutano wa hadhara uliofanyika Ellipse mnamo Januari 6, mlikuwa katika Ikulu ya Marekani siku hiyo, na mlikuwa na Trump alipozungumza kwenye mkutano wa “Stop the Steal”, taarifa inasema.

"Kamati Teule inataka kufahamu kwa undani kila kitu kilichotokea katika Ikulu ya Marekani Januari 6 na siku chache kabla. Tunahitaji kujua kwa uhakika ni jukumu gani Rais wa zamani na wasaidizi wake walitekeleza katika kusimamisha kuhesabiwa kwa kura za uchaguzi na kama kulikuwa na mawasiliano na mtu yeyote nje ya Ikulu ya Marekani anayejaribu kupindua matokeo ya uchaguzi" Bennie Thompson, Seneta wa Chama cha Democrat kutoka Jimbo la Mississippi ambaye ni mwenyekiti wa jopo hilo, amesema katika taarifa.

Wito huo wa Jumanne kwa maafisa wa zamani wa Serikali ya Trump unakuja kufuatia wito mwingine uliotolewa Jumatatu kwa washirika sita wa Trump, akiwemo meneja wake wa kampeni ya uchaguzi wa Mwaka 2020 Bill Stepien, mshauri mkuu wa kampeni hiyo Jason Miller, mshauri wa zamani wa usalama wa kitaifa Michael Flynn na wengine watatu.

Aidha, siku ya Jumanne pia, Ofisi Maalum ya Kisheria yenye jukumu la kuchunguza na kuandaa mashtaka dhdi ya makosa ya umma, ilisema katika ripoti yake kwamba maafisa 13 wa serikali ya Trump walifanya kampeni za kutaka Trump achaguliwe tena kuwa rais ikiwa ni kukiuka sheria inayojulikana kama Sheria ya Hatch ambayo imeundwa kukataza aina hii ya matumizi mabaya ya ofisi za umma.

Maafisa hao wa zamani ni pamoja na mkwe wa Trump na mshauri mkuu Jared Kushner, Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje Mike Pompeo, Mshauri wa zamani wa Usalama wa Taifa Robert O'Brien, Mkuu wa zamani wa Ikulu ya White House Mark Meadows, Kaimu Katibu wa zamani wa Usalama wa Ndani Chad Wolf na wengine. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha