Rais Xi Jinping asisitiza ustawishaji wa Sehemu ya Kaskazini Mashariki mwa China

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Agosti 19, 2022
Rais Xi Jinping asisitiza ustawishaji wa Sehemu ya Kaskazini Mashariki mwa China
Rais Xi Jinping wa China, akipewa maelezo kuhusu jitihada za serikali za mitaa katika kuhimiza uvumbuzi wa sayansi na teknolojia kwenye kampuni ya biashara wakati alipotembelea maonyesho ya Kampuni ya "Siasun Robot and Automation" huko Shenyang, Mkoa wa Liaoning, Kaskazini Mashariki mwa China, Agosti 17, 2022. Xi alifanya ziara ya ukaguzi huko Liaoning kuanzia Jumanne hadi Jumatano. (Xinhua/Ju Peng)

SHENYANG - Rais Xi Jinping amesisitiza kuwepo kwa hali zaidi ya uwajibikaji na juhudi katika kustawisha sehemu ya Kaskazini Mashariki mwa China katika zama mpya.

Katika ziara yake ya ukaguzi kwenye Mkoa wa Liaoning kuanzia Jumanne hadi Jumatano, Xi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya Kijeshi ya China, alitoa wito wa kuweka mikakati mipya katika ustawishaji na maendeleo ya Mkoa wa Liaoning.

Xi ametoa wito wa kuratibu mapambano dhidi ya UVIKO-19 na maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kuoanisha mahitaji ya maendeleo na usalama, kutekeleza kikamilifu na kwa uaminifu dhana mpya ya maendeleo, na kuhimiza kwa uthabiti maendeleo ya kiwango cha juu.

Wakati wa ukaguzi huo, Xi alifanya ziara katika miji ya Jinzhou na Shenyang, ambako alitembelea maeneo kadhaa, ikiwa ni pamoja na kumbukumbu ya mapinduzi, mradi wa usimamizi wa mto na ziwa, kampuni ya biashara, na eneo la makazi.

Huku akisisitiza kwamba hakuna fikra za kisiasa ambazo ni muhimu zaidi kuliko watu, Xi alisema kwamba maadamu CPC kinadumisha uhusiano wake na watu, kinapumua hewa sawa na watu, kinapata hatima sawa, na kushikamana nao, kinaweza kupata uwezo wa kushinda ugumu wowote.

Xi ameeleza bayana kuwa watu wa Kaskazini Mashariki mwa China walijitolea mengi kwa ajili ya ushindi wa mapigano ya Liaoshen na ukombozi wa Kaskazini Mashariki mwa China, na walitoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya China Mpya na ushindi katika Vita vya Kupinga Mabavu na Usaidizi wa Kijeshi wa Marekani kwa Korea. Xi alisema hili halitasahaulika kamwe na CPC na watu wa China.

“Kamwe hatutakubali nchi yetu ya kijamaa ibadili asili yake. Wala watu hawataweza,” amesema Xi.

Katika ziara yake kwenye mbuga ya pori tengefu huko Jinzhou, Xi alisema, dhana ya maendeleo ya kijani inapaswa kutumika kwa uhifadhi wa ikolojia, uboreshaji wa mazingira, uzalishaji na utengenezaji wa bidhaa, maendeleo ya miji, maisha ya watu, na mambo mengine ili kuharakisha ujenzi wa China nzuri.

Xi alisikiliza ripoti kuhusu juhudi za kudhibiti mafuriko katika mkoa huo, ambapo mvua kubwa katika majira ya joto iliharibu mashamba na mali za watu na karibu watu 200,000 walilazimika kuyahama makazi yao.

Alisisitiza kuwa serikali za mitaa lazima zibuni mipango ifaayo ya kukarabati na kujenga upya baada ya maafa ili kuwasaidia watu kurejea kwenye uzalishaji na kurejesha maisha yao haraka iwezekanavyo.

Rais Xi ametoa wito wa juhudi za kuimarisha uwezo wa kuzuia na kukabiliana na mafuriko na majanga ya kijiolojia, pamoja na uokoaji wa dharura na uwezo wa kutoa misaada.

Huku akieleza kuwa sehemu za China zinakabiliwa na ukame mkali, Xi pia amehimiza juhudi za kukabiliana na ukame.

Katika bustani ya umma huko Jinzhou, Xi aliwaambia wakazi kwamba mambo ya kisasa yenye umaalumu wa China yanaangazia ustawi kwa watu wote, siyo wachache tu. Pia yanajidhihirisha kwa maendeleo yenye usawa na yenye kupiga hatua katika nyenzo na maadili ya kitamaduni.

“Kamati Kuu ya CPC imetilia maanani sana ustawishaji wa sehemu ya Kaskazini Mashariki mwa nchi,” Xi alisema. "Tuna imani kamili na matarajio ya ustawishaji kamili wa Kaskazini Mashariki katika zama mpya."

Katika ziara yake kwenye Kampuni ya "Siasun Robot and Automation" katika Mji Shenyang, ambao ni mji mkuu wa Mkoa wa Liaoning, siku ya Jumatano, Xi alionyesha uthibitisho wa maendeleo yaliyofanywa na kampuni hiyo katika uvumbuzi wa kujitegemea na maendeleo ya kiviwanda.

Amesisitiza kuwa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China imeweka umuhimu katika kufanya uvumbuzi wa kujitegemea, ambao utahimiza nchi yetu kuendelezwa kuwa nchi yenye nguvu ya kiuchumi na nchi yenye nguvu ya utengenezaji wa bidhaa bora.

Xi pia alitembelea eneo la Makazi ya Mudan katika Wilaya ya Huanggu. Eneo hilo la makazi lilijengwa katika miaka ya 1980 na ni eneo la makazi yenye familia zaidi ya 3,000, limekuwa kielelezo cha utawala wa mashinani baada ya kufanyiwa ukarabati wa miundombinu na uboreshaji wa huduma katika miaka ya hivi karibuni. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha