UNESCO yafungua Mkutano wa 17 wa Ulinzi wa Urithi wa Utamaduni Usioshikika

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Novemba 29, 2022
UNESCO yafungua Mkutano wa 17 wa Ulinzi wa Urithi wa Utamaduni Usioshikika
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Audrey Azoulay akizungumza kwenye Mkutnao wa 17 wa Kamati ya Kiserikali ya UNESCO ya Kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika katika mji mkuu wa Morocco Rabat, Novemba 28, 2022. Wajumbe kutoka nchi wanachama 180 wanahudhuria mkutano huo, unaofanyika kuanzia Novemba 28 hadi Desemba 3. (Picha na Aissa/Xinhua)

RABAT – Mkutano wa 17 wa Kamati ya Kiserikali ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) wa Kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika umeanza Jumatatu katika mji mkuu wa Morocco, Rabat.

Wajumbe kutoka nchi wanachama 180 wanahudhuria mkutano huo, unaofanyika kuanzia Novemba 28 hadi Desemba 3.

Wakati wa mkuano huo kamati itatathmini zaidi ya mapendekezo 50 yaliyowasilishwa na Nchi Wanachama ili kuandikwa kwenye Orodha za Mkataba, ikiwa ni pamoja na mbinu za jadi za usindikaji wa chai na desturi zinazohusiana nazo za kijamii nchini China.

Mfalme wa Morocco Mohammed VI alitoa hotuba ya ukaribisho katika ufunguzi wa mkutano huo, ambayo ilisomwa na Katibu Mkuu wa Serikali ya Morocco Mohamed El Hajoui.

“Mkutano huo unafanyika miaka 19 baada ya kupitishwa kwa Mkataba wa kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika, chombo ambacho kimewezesha kupatikana kwa maendeleo makubwa katika maeneo mbalimbali yanayohusu urithi wa utamaduni usioshikika,” amesema mfalme katika hotuba yake.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya haraka yanayoathiri Dunia leo, imekuwa muhimu kuzingatia ulinzi wa urithi usioshikika wa nchi kote duniani na kuchukua hatua za kuhifadhi, ameongeza.

Hafla ya ufunguzi wa mkutano huo pia ilihudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO Audrey Azoulay, Balozi na Mjumbe Mkuu wa Ufalme wa Morocco kwenye UNESCO, na Katibu wa Mkataba wa Kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika, Tim Curtis.

Mkataba wa Kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika ulipitishwa katika Mkutano Mkuu wa 32 wa UNESCO Oktoba 17, 2003, ili kulinda urithi wa utamaduni usioshikika duniani.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha