Ripoti yaonyesha Marekani hutumia kampuni za teknolojia zinazodhibiti mtandao kupeleleza Dunia

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Machi 31, 2023
Ripoti yaonyesha Marekani hutumia kampuni za teknolojia zinazodhibiti mtandao kupeleleza Dunia
Picha ya kumbukumbu iliyopigwa Machi 18, 2015 ikimuonyesha Edward Snowden kwenye skrini ya kamera wakati wa mahojiano ya moja kwa moja ya mbali kwenye maonyesho ya CeBIT 2015, ambayo ni maonyesho makubwa zaidi ya biashara ya teknolojia za upashanaji wa habari na mawasiliano duniani (TEHAMA), huko Hanover, Ujerumani. (Xinhua/Zhang Fan)

CAIRO - Huku ikishinikiza kupigwa marufuku kwa mtandao wa TikTok kwa madai kwamba China inatumia programu hiyo maarufu kuwapeleleza Wamarekani, serikali ya Marekani yenyewe inaipeleleza Dunia kwa kutumia kampuni za teknolojia ambazo zinadhibiti ipasavyo mtandao wa intaneti wa kimataifa, inasema ripoti iliyochapishwa kwenye tovuti ya habari ya Lugha ya Kiingereza ya Shirika la Habari la Al Jazeera.

Serikali ya Marekani inaruhusu mashirika yake ya kijasusi "kufanya upelelezi bila ruhusa " kwenye barua pepe, simu na mawasiliano mengine ya mtandaoni ya raia wa kigeni, imesema ripoti hiyo iliyochapishwa Jumanne.

“Ikilinganishwa na nchi nyingine, Washington ina faida ya kuwa na mamlaka juu ya idadi ndogo ya kampuni kubwa ambazo zinaendesha vyema mtandao wa kisasa wa intaneti, ikiwa ni pamoja na Google, Meta, Amazon na Microsoft,” inasema ripoti hiyo.

"Ni kesi ya 'sheria kwa ajili yako lakini si kwa ajili yangu,'" Asher Wolf, mtafiti wa teknolojia na mtetezi wa faragha anayeishi Australia, amenukuliwa akisema kwenye ripoti hiyo.

Ripoti hiyo inasema, Marekani ililenga "watu wasio wa Marekani" 232,432 kwa upelelezi Mwaka 2021, mwaka ambao ni wa hivi karibuni kwa takwimu zake kupatikana.

Ripoti hiyo imesema, Muungano wa Asasi zinazotetea Uhuru wa Kiraia wa Marekani (ACLU) unakadiria kuwa serikali ya Marekani imekusanya mawasiliano zaidi ya bilioni 1 kwa mwaka tangu Mwaka 2011.

Ripoti hiyo inabainisha kuwa, kumekuwa na baadhi ya viashilio kwamba maofisa wa Marekani wanaiona China, badala ya TikTok yenyewe, kama suala la kuamua kufuatilia.

Hatua za Marekani za kuiwekea vikwazo TikTok zinaonekana kuwa "za kisiasa zaidi kuliko sera nzuri," Vedran Sekara, profesa msaidizi katika Chuo Kikuu cha Teknolojia za Habari cha Copenhagen, amenukuliwa akisema.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha