Watanzania 29 washinda kwenye mashindano ya stadi za kufundisha yaliyoandaliwa na taasisi za kitaaluma za Tanzania na China

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 18, 2023
Watanzania 29 washinda kwenye mashindano ya stadi za kufundisha yaliyoandaliwa na taasisi za kitaaluma za Tanzania na China
Mwanafunzi (kushoto, mbele) akipokea tuzo kwenye hafla ya utoaji tuzo za mashindano ya stadi za kufundisha jijini Dar es Salaam, Tanzania, Aprili 17, 2023. (Picha na Herman Emmanuel/Xinhua)

DAR ES SALAAM - Wanafunzi 29 kati ya 105 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinachomilikiwa na serikali ya Tanzania Jumatatu wamepewa tuzo baada ya kushinda Mashindano ya Kwanza ya Stadi za Kufundisha.

Mashindano hayo yaliyoandaliwa kwa pamoja na Chuo cha Elimu (SoED) katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Kituo cha Pamoja cha Utafiti wa Elimu cha China na Afrika (SA-JoCER), yanalenga kuwawezesha walimu wanafunzi kuonesha umahiri, uwezo na ubunifu wao.

Eugenia Kafanabo, Mkuu wa Shule ya Elimu (SoED) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema mashindano hayo yanalenga walimu wanafunzi ambao wako katika mwaka wao wa pili na wa tatu wa masomo. "Mashindano ya stadi za kufundisha yalilenga kuongeza uelewa wa umuhimu wa vitendo na kuboresha miundo ya ufundishaji."

Kafanabo amesema kwenye Ukumbi wa Taasisi ya Confucius katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwamba, mashindano hayo yamehusisha masomo 10 tofauti ambayo yalichaguliwa kutoka katika mihtasari ya shule za sekondari, yakiwemo masomo ya biolojia, kemia, fizikia, hisabati, uraia, historia, jiografia, Kiswahili, Kiingereza na masomo ya lugha ya Kichina.

“Mashindano haya yanaweza kuwa kiingilio cha kuwaleta pamoja wadau wote husika kama muungano wa kuchangia ubora wa elimu ya walimu,” amesema Eilleen Xu, Mratibu wa SA-JoCER, iliyoanzishwa kwa pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang cha China.

Mkurugenzi wa Elimu ya Msingi katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya Tanzania, Venance Manori, amekipongeza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang cha China kwa kuandaa mashindano hayo, akisema mashindano hayo yataboresha ujuzi wa kufundisha kwa walimu wa Tanzania.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha