Mikataba ya uwekezaji yenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 10 yatiwa saini kwenye maonyesho ya RCEP katikati mwa China

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 09, 2023
Mikataba ya uwekezaji yenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 10 yatiwa saini kwenye maonyesho ya RCEP katikati mwa China
Picha hii iliyopigwa Tarehe 5 Mei 2023 ikionyesha ukumbi wa Maonyesho ya Kwanza ya Kiuchumi na Biashara ya Hunan (Huaihua) ya Ushirikiano Kamili wa Kiuchumi wa Kikanda (RCEP) katika Mji wa Huaihua, Mkoa wa Hunan, Katikati mwa China. (Xinhua/Yu Chunsheng)

CHANGSHA - Mikataba ya uwekezaji kwa ajili ya miradi jumla ya 113 yenye uwekezaji wa pamoja wenye thamani ya takriban yuan bilioni 75 (kama dola bilioni 10.84 za Kimarekani) imetiwa saini wakati wa maonyesho ya Ushirikiano Kamili wa Kiuchumi wa Kikanda (RCEP) ya kiuchumi na kibiashara yaliyofanyika katika Mkoa wa Hunan, katikati mwa China.

Maonyesho hayo yaliyoanza Mei 4 katika Mji wa Huaihua mkoani humo yametumika kama jukwaa jipya la mabadilishano na ushirikiano kati ya nchi na maeneo washiriki wa RCEP na maeneo ya China ya ngazi ya mkoa kwenye Ukanda Mpya wa Kimataifa wa Biashara ya Nchi kavu na Baharini, ambao ni njia ya biashara na uchukuzi wa bidhaa iliyojengwa kwa pamoja na maeneo ya ngazi ya mkoa ya Magharibi mwa China na nchi wanachama wa Jumuiya ya Nchi za Asia Kusini Mashariki (ASEAN), kwa mujibu wa mratibu.

Maonyesho hayo yaliyofanyika kwa siku nne yamevutia zaidi ya kampuni 600 maarufu na zaidi ya wanunuzi 1,000 kutoka ndani na nje ya China, zikiwemo kampuni 112 kutoka nchi na maeneo mengine 14 washiriki wa RCEP.

Pamoja na shughuli mbalimbali za nje ya mtandao na mtandaoni, maonyesho hayo yalikuwa na zaidi ya aina 2,000 za bidhaa zilizoangaziwa kutoka nchi na maeneo washiriki wa RCEP zilizoonyeshwa kwenye kituo cha kimataifa cha mikutano cha mji huo.

Huaihua ndiyo mji pekee wa mkoa kando ya ukanda huo na kituo cha kukusanya mizigo kwa nchi za ASEAN. 

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha