

Lugha Nyingine
Kituo Kikuu cha Vyombo vya Habari cha Michezo ya Asia ya Hangzhou chaanza kufanya kazi rasmi
![]() |
Picha iliyopigwa Septemba 1 ikionyesha sehemu ya nje ya Kituo Kikuu cha Vyombo vya Habari cha Michezo ya Asia ya Hangzhou. (Xinhua/Xu Yu) |
HANGZHOU – Ikiwa imebakia takriban wiki moja kabla ya kuanza kwa Michezo ya 19 ya Asia ya Hangzhou, Kituo Kikuu cha Vyombo vya Habari (MMC) cha michezo hiyo kimeanza kufanya kazi rasmi siku ya Jumatatu.
Kikipatikana karibu na uwanja mkuu wa Kituo cha Michezo ya Olimpiki cha Hangzhou, uwanja ambao utatumika kwa hafla ya ufunguzi wa michezo hiyo, eneo la Kituo Kikuu cha Vyombo vya Habari ni la mita za mraba karibu 50,000. Kituo hiki kimegawanywa katika sehemu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Kituo Kikuu cha Waandishi wa Habari (MPC) na Kituo cha Kimataifa cha Utangazaji (IBC).
Ndani ya kituo hicho, wafanyakazi wa vyombo vya habari wanaweza kupata huduma mbalimbali za haraka na bora katika kituo cha matibabu, duka la vitabu, na ofisi ya posta.
Eneo la maonyesho ya kitamaduni, lililo katika ukumbi wa kituo hicho, linaonyesha sanaa za aina mbalimbali za China, ikiwa ni pamoja na picha za uchoraji wa jadi na vyombo vya kauri. Maonyesho haya yameonesha sifa maalum za tamaduni za China na Hangzhou.
Michezo ya 19 ya Asia imepangwa kufanyika Hangzhou, Mji Mkuu wa Mkoa wa Zhejiang, Mashariki mwa China, kuanzia Septemba 23 hadi Oktoba 8 na itahusisha mashindano ya jumla ya michezo 40.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma