Uturuki kufanya juhudi kwa ajili ya makubaliano ya kudumu huko Gaza: Erdogan

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Novemba 30, 2023
Uturuki kufanya juhudi kwa ajili ya makubaliano ya kudumu huko Gaza: Erdogan
Picha hii iliyopigwa Novemba 29, 2023 ikionyesha majengo yaliyobomolewa katika Mji wa Gaza. (Picha na Mohammed Ali/Xinhua)

ANKARA - Baada ya wiki kadhaa za mashambulizi ya Israel katika Ukanda Gaza ambayo hadi sasa yamewaua Wapalestina takribani 15,000 katika kulipiza kisasi dhidi ya mashambulizi ya Oktoba 7 yaliyofanywa na Kundi la Hamas na kuwaua Waisraeli takriban 1,200 huku watu zaidi ya 200 wakitekwa nyara na sasa usimamishaji vita wa kibinadamu umeendelea kwa siku 6, Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan amesema Jumatano kwamba nchi yake itaongeza juhudi zake za kuwaachilia huru mateka na kufikia makubaliano ya kudumu ya kusimamisha vita katika Ukanda wa Gaza.

"Tutaharakisha mawasiliano yetu ili kuwaachilia huru mateka na kufanya usimamishaji vita kuwa wa kudumu," Erdogan amesema kwenye Mtandao wa X, ambao zamani ulijulikana kwa jina la Twitter, wakati wa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina.

"Tunatumai, mipango yetu itaendelea kwa njia ya pande nyingi katika siku zijazo," amesema.

Kwa mujibu wa Erdogan Serikali ya Uturuki inaendelea kupeleka misaada ya kibinadamu kwa watu wa Gaza na hadi sasa imetuma ndege 12 za misaada na meli moja nchini Misri.

Meli ya pili iliyobeba misaada ya kibinadamu yenye uzito wa tani 1,500 imefunga safari mapema Jumatano, kwa mujibu wa rais huyo wa Uturuki.

Uturuki imepokea wagonjwa wengine 23 wa Gaza, pamoja na wenzao 21, kwa ajili ya matibabu katika mji mkuu, Ankara mwishoni mwa Jumatano.

Waziri wa Afya wa Uturuki Fahrettin Koca, ambaye amewakaribisha katika uwanja wa ndege wa Etimesgut mjini Ankara, amesema Uturuki hadi sasa imepokea watu jumla ya 200 kutoka Gaza, wakiwemo wagonjwa 114 na ndugu zao 86.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha