Waziri Mkuu wa Israel Netanyahu akataa pendekezo la Hamas la kusimamisha mapigano huko Gaza

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Februari 08, 2024
Waziri Mkuu wa Israel Netanyahu akataa pendekezo la Hamas la kusimamisha mapigano huko Gaza
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari katika ofisi ya Waziri Mkuu mjini Jerusalem, Februari 7, 2024. (Marc Israel Sellem/JINI kupitia Xinhua)

JERUSALEM - Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kwenye mkutano na waandishi wa habari Jumatano amekataa pendekezo la Kundi la Hamas la kusimamisha mapigano katika Ukanda wa Gaza akisema "Kukubali matakwa danganyifu ya Hamas kutasababisha mauaji mengine makubwa," na amesisitiza tena msimamo wake kwamba Israel itaendelea kufanya vita hadi "ushindi kamili" dhidi ya Hamas.

Kauli hizi za Netanyahu zimekuja saa chache baada ya Hamas, kundi lenye siasa kali la Palestina wanaoendesha Gaza, kuwasilisha orodha ya masharti kujibu pendekezo la kusimamisha mapigano lililosuluhishwa na Qatar, ambalo linahusisha mabadilishano ya mateka wa Israel kwa wafungwa wa Palestina na ujenzi upya wa Gaza, ambayo imeharibiwa katika mashambulizi ya Israeli. Hamas pia inataka Israel kuondoa kabisa majeshi yake na kukomesha vita vinavyoendelea, ikipendekeza mpango wa kusimamisha mapigano unaojumuisha vipindi vitatu, ambavyo kila moja itadumu kwa siku 45.

"Usiku wa leo, nimekuja kuwaambia jambo moja: Tuko njiani kuelekea ushindi kamili. Ushindi unaweza kupatikana. Siyo suala la miaka lakini la miezi," Netanyahu amesema.

Netanyahu amesema, tangu Oktoba 7, 2023, Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limeshaua au kujeruhi watu wenye silaha 20,000 huko Gaza, ambao ni "zaidi ya nusu ya vikosi vya Hamas."

"Tumeiagiza IDF, ambayo sasa iko Khan Younis, ngome ya mwisho ya Hamas, kujiandaa kufanya oparesheni huko Rafah pia," amesema.

Netanyahu amesema alimwambia Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken, kwenye mkutano wao mjini Jerusalem mapema siku hiyo ya Jumatano, kwamba baada ya Hamas " kuangamizwa," Gaza inapaswa kubaki bila shughuli zozote za kijeshi ili kuhakikisha haitakuwa tishio la usalama kwa Israeli.

"Inamaanisha kuwa Israel itakaa Gaza," amesema.

Wizara ya Afya inayoendeshwa na Hamas ilisema Jumatano kuwa, Vita vya Israel na Hamas hadi sasa vimewafanya watu 27,708 kupoteza maisha huko Gaza.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha