Misri yaandaa mkutano wa kimataifa kujadili mageuzi ya nishati mpya

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Februari 20, 2024
Misri yaandaa mkutano wa kimataifa kujadili mageuzi ya nishati mpya
Watu wakitembelea Maonyesho ya Nishati ya Misri huko Cairo, Misri, Februari 19, 2024. (Xinhua/Ahmed Gomaa)

CAIRO – Mkutano wa Kimataifa wa Nishati umeanza siku ya Jumatatu nchini Misri kujadili changamoto na fursa za kuhamia kwenye nishati mpya ukiambatana na Maonyesho ya Nishati ya Misri (EGYPES 2024) ambayo yatafanyika Februari 19 hadi 21, yakiwa na kaulimbiu isemayo "Kuhimiza mageuzi ya Nishati, Usalama, na Kuondoa kaboni" huku teknolojia mpya na uvumbuzi katika sekta ya mafuta, gesi na nishati zikitarajiwa kuonyeshwa.

Rais wa Misri Abdel-Fattah al-Sisi amewakaribisha mamia ya wataalamu na maafisa wanaoshiriki katika mkutano huo na kusema kuwa maonyesho katika mkutano huo yanatazamia teknolojia yenye gharama kubwa na uwekezaji mkubwa.

Waziri wa Petroli wa Misri Tarek El-Molla amesema mkutano huo unafanyika wakati Dunia inakabiliwa na tishio kubwa la mabadiliko ya tabianchi ambayo yanahatarisha mustakabali wa maendeleo endelevu.

Amesisitiza ahadi ya Misri kwa mwenendo wa kimataifa wa kutumia haidrojeni na vyanzo vya nishati safi, akisema maonyesho ya EGYPES 2024 yatasaidia kujenga mustakabali bora wa sekta ya nishati na rasilimali watu inayohusika.

Pia amehimiza misaada zaidi na ufadhili wenye masharti nafuu kwa nchi za Afrika ili kutimiza mageuzi ya nishati ulio wa haki na salama, kwa ushirikiano na taasisi za kimataifa.

Mkutano huo utajumuisha mijadala zaidi ya 80 pamoja na watu zaidi 300 kujadili kuhusu mada sita muhimu, zikiwemo usalama wa nishati, kuondoa kaboni, maendeleo ya kidijitali, uvumbuzi, uwekezaji na rasilimali watu.

Kupitia hotuba kuu, mijadala ya jopo na mahojiano, mkutano huo utashughulikia masuala muhimu zaidi na fursa zinazokabili sekta ya mafuta, gesi na nishati katika ngazi ya kikanda na kimataifa.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha