Rais Xi asema China itafanya ushirikiano na Micronesia katika miundombinu na mabadiliko ya tabianchi

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 10, 2024
Rais Xi asema China itafanya ushirikiano na Micronesia katika miundombinu na mabadiliko ya tabianchi
Rais Xi Jinping wa China akisalimiana na Rais wa Nchi ya Shirikisho la Majimbo ya Micronesia Wesley W. Simina mjini Beijing, China, Aprili 9, 2024. (Xinhua/Li Xueren)

BEIJING - Rais wa China Xi Jinping amesema siku ya Jumanne kwenye mazungumzo yake na Rais wa Nchi ya Shirikisho la Majimbo ya Micronesia Wesley W. Simina kwamba China na Micronesia zinapaswa kuimarisha ushirikiano katika miundombinu, na China ingependa kutoa msaada kwa nchi hiyo ya kisiwa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

China inaunga mkono Micronesia katika kulinda mamlaka ya nchi na uhuru wake, kufuata njia ya maendeleo inayoendana na hali halisi ya nchi, kustawisha uchumi wake na kuboresha maisha ya watu, Rais Xi amesema.

Huku akieleza kuwa mwaka huu ni maadhimisho ya miaka 35 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya China na Micronesia, China ingependa kusukuma mbele maendeleo ya uhusiano kati ya nchi hizo mbili.

Ametoa wito kwa pande zote mbili kuharakisha ushirikiano chini ya Pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja, kuongeza ushirikiano katika miundombinu, na kuimarisha mawasiliano katika sekta za utamaduni, afya, elimu na serikali za mitaa. Amewakaribisha vijana zaidi kutoka Micronesia kuja kusoma nchini China.

Rais Xi amesema China ingependa kutoa msaada kwa Micronesia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ndani ya mfumo wa ushirikiano wa Kusini na Kusini na kuimarisha uratibu na ushirikiano na nchi hiyo ya kisiwa ndani ya Umoja wa Mataifa na Jukwaa la Visiwa vya Pasifiki ili kutekeleza kwa pamoja ushirikiano wa pande nyingi.

Rais Xi amesema uhusiano wa China na nchi za visiwa ulianzishwa kwenye msingi wa kusaidiana ndani ya mfumo wa ushirikiano wa Kusini na Kusini, na haulengi upande wa tatu wala haupaswi kuingiliwa na upande wowote.

China inashikilia kuwa nchi yoyote inayotaka kuendeleza uhusiano na nchi za visiwa vya Pasifiki inapaswa kuheshimu machaguo yao ya kujiamulia, kuweka maendeleo katika kipaumbele cha juu, na kutilia maanani uwazi na ujumuishaji.

"China ingependa kuendelea kutoa uungaji mkono kwa maendeleo ya nchi za visiwa kwa iwezavyo na kufanya ushirikiano wa pande tatu au wa pande nyingi," Rais Xi amesema.

Kwa upande wake, Simina ambaye yuko katika ziara ya kiserikali nchini China kuanzia Aprili 5 hadi 12 amesema Micronesia inatambua kwamba Taiwan ni sehemu isiyoweza kutengwa ya ardhi ya China, na inaunga mkono msimamo wa China juu ya masuala yanayohusiana na maslahi yake makuu kama vile Taiwan, Hong Kong, Xinjiang na Xizang.

Simina ameishukuru China kwa msaada wake muhimu kwa Micronesia na nchi nyingine za visiwa vya Pasifiki kwa maendeleo yao ya kiuchumi na kijamii kwa miaka mingi.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha