Teknolojia ya Juncao ya China yawezesha wajasiriamali wa Rwanda

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 22, 2024
Teknolojia ya Juncao ya China yawezesha wajasiriamali wa Rwanda
Nyambo Obed akionyesha uyoga uliolimwa kwenye banda lake karibu na Muhanga katika mkoa wa Kusini, Rwanda, Aprili 6, 2024. (Xinhua/Dong Jianghui)

KIGALI - Katika wilaya ya Kabuye ya Kigali, mji mkuu wa Rwanda, banda la uyoga lenye shughuli nyingi linafanya kazi kwa taratibu. Wafanyakazi wawili wanachanganya kwa uangalifu unga wa nyasi ya kuvu, maganda ya mbegu za pamba na maji katika mashine ya kuchanganyia, huku mwingine akiendesha mashine ya kuziweka kwenye mfuko wa plastiki, ili kuhakikisha kila mfuko umejazwa mchanganyiko unaofaa kwa kuzalisha uyoga.

“Baada ya kuisafisha mifuko hiyo kwenye joto la juu, tunaipandikiza vimelea katika mazingira yasiyo na uchafu. Inachukua takribani siku 35 kwa vimelea vya uyoga kuota kwenye mirija yote, kisha inakuwa tayari kupandikizwa,” amefafanua Leonidas Mushimiyimana, mmiliki wa banda hilo.

Mushimiyimana, mwenye umri wa miaka 42, ambaye ni baba wa watoto wawili, amesimulia safari yake ya kuanzia chuo kikuu hadi ujasiriamali, akisukumwa na shauku ya kupata ajira ya muda mrefu na kutafuta fursa nzuri.

Mafanikio yake yalipatikana mwaka 2013, kutokana na juhudi za ushirikiano kati ya serikali ya Rwanda na China. Kupitia ushirikiano huu, Mushimiyimana alipata mafunzo ya teknolojia ya Juncao katika Chuo Kikuu cha Kilimo na Misitu cha Fujian, Kusini Mashariki mwa China.

Aliporejea Rwanda, Mushimiyimana alianzisha Kampuni ya DEYI, akianzisha mradi wake wa kuzalisha uyoga. Ndani ya miaka miwili, biashara yake ilipanuka, na kuanzishwa banda la sasa, ikiuza uyoga kwa Kigali na kuusafirisha nchi jirani kama vile Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Juncao, nyasi mseto iliyopandwa kwa miongo kadhaa ya utafiti wa kisayansi wa China, imejitokeza kuwa rasilimali ya kilimo yenye kazi nyingi.

"Juncao inajulikana kama 'dawa ya kuleta furaha' nchini Rwanda," amesema Zheng Ruijin, mtaalam wa kilimo katika Kituo cha Kielelezo cha Teknolojia ya Kilimo cha China na Rwanda.

Licha ya kilimo cha uyoga, majani, mashina na mizizi yake hutumika katika ulinzi wa kiikolojia, kupambana na mmomonyoko wa udongo na hali ya kuenea kwa jangwa huku vikitumika kama lishe ya mifugo na kuku pia.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2011, kituo hiki kimesaidia kampuni na vyama vya ushirika zaidi ya 50 vinavyohusika na kuzalisha uyoga nchini Rwanda. Imeendesha kozi za mafunzo 47, zikiwapa utaalamu wenyeji karibu 1,800 juu ya teknolojia ya Juncao.

Leo, teknolojia hiyo inanufaisha wakulima zaidi ya 4,000 wa Rwanda, na hivyo kuongeza ajira zaidi ya 30,000 kwenye mnyororo wa thamani wa kilimo.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha