

Lugha Nyingine
Kituo cha Utamaduni cha China huko Budapest, Hungary chafunguliwa rasmi (2)
BUDAPEST - Kituo cha Utamaduni cha China mjini Budapest, Hungary kimefunguliwa rasmi siku ya Alhamisi, kwa shughuli ya ufunguzi iliyohusisha maonyesho ya picha na maonyesho ya ustadi wa chai ambapo Waziri wa Utamaduni na Ubunifu wa Hungary Janos Csak alizungumza kwenye hafla hiyo juu ya urafiki wa kudumu na wa kuheshimiana kati ya Hungary na China.
“Kufunguliwa kwa kituo hicho kunaashiria hatua nyingine kubwa katika ushirikiano wetu unaoweka mkazo katika maeneo ya kiuchumi, kiutamaduni, kibiashara na mambo ya fedha,” amesema.
Ameongeza kuwa, kituo hicho kipya cha utamaduni kitaongeza uelewa wa watu wa Hungary kuhusu utamaduni wa China, na kuimarisha uhusiano wa pande mbili.
Wakati huo huo, Balozi wa China nchini Hungary Gong Tao ametoa shukrani kwa uungaji mkono aliopokea kutoka serikali ya Hungary, na kuelezea matumaini kwamba kituo hicho kitasaidia mawasiliano ya utamaduni.
"Ingawa China na Hungary zimetenganishwa na umbali mkubwa, urafiki kati ya watu wetu una historia ndefu na mustakabali mzuri," ameongeza.
Naye Mkurugenzi wa Kituo cha Utamaduni cha China mjini Budapest Jin Hao aliwakaribisha wageni na kushukuru juhudi za ushirikiano zilizopelekea kufunguliwa kwa kituo hicho.
Hafla hiyo iliendelea kwa kuzindua bamba lenye jina la kituo hicho, kuonyesha ustadi wa chai na kutazama maonyesho ya picha yaliyopewa jina la "Tafakari ya Njia ya Hariri - China Kupitia Macho ya Wapiga Picha wa Hungary."
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma