China yaitaka Marekani kusitisha hatua za kibaguzi

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 20, 2025

BEIJING - Wizara ya Biashara ya China imeilaani Marekani jana Jumatatu kwa kutumia vibaya hatua za udhibiti wa mauzo ya nje zinazolenga bidhaa za chipu za China, ikiitaka nchi hiyo kurekebisha mara moja makosa yake na kuacha hatua za kibaguzi dhidi ya China.

Akizungumzia tangazo lililorekebishwa la Marekani kuhusu bidhaa za chipu za China, msemaji huyo amesema kwamba tangazo hilo kimsingi bado lina hatua za kibaguzi na litapotosha soko.

Msemaji huyo amesema, Marekani imetumia vibaya hatua zake za udhibiti wa mauzo ya nje na kuweka vizuizi vikali zaidi kwa bidhaa za chipu za China kwa madai yasiyo na msingi hata kidogo, na China inapinga vikali vitendo hivyo vya umwamba vya upande mmoja.

Amesema, “Vitendo hivyo vya Marekani vimekiuka vibaya haki na maslahi halali ya kampuni za China, vimetishia usalama na utulivu wa minyororo ya kimataifa ya viwanda na utoaji wa bidhaa za semiconductor, na kuvuruga uvumbuzi wa kiteknolojia duniani”.

Ameutaka upande wa Marekani kujiunga pamoja na China katika kulinda mwafaka uliofikiwa katika mazungumzo ya ngazi ya juu ya Geneva, na kuhimiza ujenzi wa uhusiano kati ya pande mbili katika sekta za uchumi na biashara ulio wa endelevu, wa muda mrefu na wenye kunufaishana ili kupata maendeleo kwa pamoja.

“Kama Marekani itaendelea kuisababishia China madhara makubwa, China itachukua hatua kithabiti kwa kulinda haki na maslahi yake halali,” amesema msemaji huyo.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha