Mamilioni ya Watu waandamana kupinga sera za uhamiaji za Marekani na vita dhidi ya Iran (3)

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Machi 30, 2026
Mamilioni ya Watu waandamana kupinga sera za uhamiaji za Marekani na vita dhidi ya Iran
Watu wakishiriki kwenye maandamano ya "Hapana Wafalme", New York, Marekani, Machi 28, 2026. (Xinhua/Zhang Fengguo)

SACRAMENTO/NEW YORK, Marekani - Mamilioni ya Wamarekani walimiminika mitaani siku ya Jumamosi wakiwa kwenye wimbi la tatu la maandamano ya "Hapana Wafalme" (No Kings) kote Marekani, wakipinga sera za utawala wa Marekani, kuanzia vita dhidi ya Iran hadi sera tata za utekelezaji wa sheria za uhamiaji.

Zaidi ya Maandamano 3,100 yalipangwa kote nchini Marekani na kufanyika katika miji mikubwa ya Marekani kama vile Washington D.C., New York, Boston, Los Angeles na San Francisco. Vyombo vya habari vya Marekani vilikadiria kuwa maandamano hayo yalihusisha takriban watu 900,000, idadi ambayo imeyafanya kuwa tukio kubwa zaidi la maandamano ya siku moja kuwahi kurekodiwa.

Waandaaji wa "Hapana Wafalme" wamesema kwamba raundi mbili zilizopita za maandamano ya amani zilivutia zaidi ya watu milioni 5 mwezi Juni na milioni 7 mwezi Oktoba 2025.

Siku ya Jumamosi, mkutano mkuu ulifanyika katika jengo la Bunge la jimbo la Minnesota mjini Saint Paul, ambapo karibu watu 100,000 walishiriki licha ya hali ya hewa ya baridi, waandaaji wamesema. Idara ya Usalama wa Barabara ya Minnesota, State Patrol imethibitisha washiriki wasiopungua 50,000.

Maandamano hayo yalilenga hasa kupinga hatua za kijeshi za Marekani dhidi ya Iran, vifo vya raia wawili wa Marekani vilivyotokea Januari ambavyo vilihusisha maafisa wa Idara ya Uhamiaji na Forodha ya Marekani (ICE) huko Minneapolis, na kile waandaaji walichokitaja kuwa ni matumizi makubwa kupita kiasi ya madaraka na utawala wa Donald Trump.

Makundi yaliyoandaa maandamano hayo ni pamoja na Indivisible, MoveOn, Muungano wa Uhuru wa Raia wa Marekani, na Shirikisho la Wafanyakazi la Marekani na Kongamano la Mashirika ya Viwanda.

Seneta huru wa Marekani Bernie Sanders, mwanasiasa kutoka jimbo la Vermont na mzungumzaji mkuu kwenye tukio la Saint Paul, alikosoa vikali sera za Marekani, akisema kuwa Wamarekani walidanganywa kuhusu vita dhidi ya Vietnam na Iraq, "na tunadanganywa leo kuhusu vita dhidi ya Iran. Vita hivi lazima viishe mara moja."

Katika Jiji la New York, maandamano yalifanyika kwenye wilaya zote tano: Bronx, Brooklyn, Manhattan, Queens na Staten Island. Katika eneo la Manhattan, makumi ya maelfu ya waandamanaji waliandamana kwenye Barabara ya Seventh Avenue siku ya Jumamosi alasiri, wakienea kwa zaidi ya mitaa 10, wakipaza sauti kaulimbiu na kubeba mabango yenye maneno "Hapana ICE," "Hapana Wafalme," na "Hapana Vita."

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha