Lugha Nyingine
Iran yakataa mpango wa Marekani wa kusimamisha mapigano, yatoa mpango wa vipengele 10 wa kukomesha vita
Shirika rasmi la habari la Iran, IRNA limeripoti jana Jumatatu kuwa Iran imekataa mpango wa amani wa vipengele 15 uliopendekezwa na Marekani, na badala yake imetoa wito wa kukomeshwa kwa kudumu kwa mgogoro huo.
Tehran imetoa jibu lake hilo kupitia Pakistan katika nyaraka yenye vipengele 10, ikirejelea uzoefu uliopita kama sababu ya kutoweza kukubali kusimamisha mapigano.
Jibu hilo linaelezea madai ya Iran, ikiwa ni pamoja na kukomesha migogoro ya kikanda, kuanzisha njia salama ya kupitia kwenye Mlango-Bahari wa Hormuz, kujenga upya maeneo yaliyoathiriwa na vita, na kuondoa vikwazo vya kimataifa.
Shirika hilo la habari la IRNA limedai kuwa mpango huo umewasilishwa kufuatia mwelekeo wa hivi karibuni katika maeneo ya magharibi na katikati mwa Iran na matokeo ambayo hayakufanikiwa ya operesheni ya utafutaji na uokoaji ya Marekani kwa kutumia helikopta na ndege, huku Rais wa Marekani Donald Trump akiongeza tena muda wa mwisho uliowekwa hapo awali na kurekebisha vitisho vya awali.
Katika mkutano na waandishi wa habari siku hiyo ya Jumatatu, Trump alilielezea jibu hilo la vipengele 10 la Iran kuwa ni "hatua muhimu" lakini akasema "haitoshi."
Pia siku hiyo ya Jumatatu, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baghaei, alisema kusimamisha mapigano kutawapa wapinzani muda wa kujipanga upya na kufanya uhalifu zaidi, na "hakuna mtu mwenye akili timamu" atakayekubali hilo.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



