IGAD na mamlaka za Djibouti zasisitiza dhamira ya kufanya uchaguzi wa kuaminika na wa amani

(CRI Online) April 08, 2026

Waangalizi wa uchaguzi kutoka Mamlaka ya Kiserikali juu ya Maendeleo ya Nchi za Afrika Mashariki (IGAD) jana Jumanne walizungumza na mamlaka za kisiasa na uchaguzi za Djibouti kabla ya uchaguzi wa rais wa wiki hii.

Katika taarifa iliyotolewa Jumanne, IGAD yenye makao yake makuu nchini Djibouti imesema ujumbe wake, unaoongozwa na Rais wa zamani wa Ethiopia Mulatu Teshome, ulifanya mashauriano muhimu na mamlaka ya Djibouti, na kusisitiza dhamira ya pamoja ya kuwa na mchakato wa uchaguzi wenye kuaminika, wa wazi na amani.

Djibouti inatarajiwa kufanya uchaguzi wake wa rais Aprili 10, huku Rais aliye madarakani sasa Ismail Omar Guelleh wa Muungano wa UMP (Union for the Presidential Majority) akikabiliana na Mohamed Farah Samatar wa chama cha UDC.

Kama sehemu ya shughuli zake, ujumbe wa IGAD ulikutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa nchi hiyo Abdoulkader Houssein Omar, Rais wa Baraza la Katiba Abdi Ismael Hersi, na Rais wa Kamisheni ya Taifa ya Haki za Binadamu Ali Soubaneh Atteyeh.

IGAD imesema majadiliano hayo yalijikita katika utayari wa kitaasisi kuendesha uchaguzi kwa ufanisi, mfumo wa kisheria wa uchaguzi, vilevile ulinzi wa haki za binadamu katika mchakato wa uchaguzi.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha