Lugha Nyingine
Wadagni aapishwa kuwa rais wa Benin (3)
![]() |
| Rais wa Benin Romuald Wadagni (kushoto) na Mkewe Nathalie Villette Wadagni wakihudhuria hafla ya kuapishwa kwa rais, Cotonou, Benin, Mei 24, 2026. (Picha na Seraphin Zounyekpe/Xinhua) |
COTONOU - Romuald Wadagni, ambaye alichaguliwa kuwa rais wa Benin katika uchaguzi wa Aprili 12, ameapishwa rasmi jana Jumapili katika Jumba la Bunge la Benin mjini Cotonou, mji mkuu wa kiuchumi wa nchi hiyo.
Hafla hiyo iliwakutanisha wageni zaidi ya 6,000, wakiwemo wakuu wa taasisi za serikali, wajumbe wa vyombo vya kikatiba, marais wa zamani Nicephore Soglo na Thomas Boni Yayi, vilevile wajumbe wa kundi la wanadiplomasia walioidhinishwa kuziwakilisha nchi na mashirika mbalimbali nchini Benin.
Mbele ya Dorothe Sossa, Mkuu wa Mahakama ya Kikatiba, mkuu huyo mpya wa nchi aliahidi kuitumikia na kuitetea Benin wakati wa muhula wake wa miaka saba wa kikatiba.
Wadagni, rais wa tano wa Benin tangu ujio wa mwanzo mpya wa kidemokrasia Februari 1990, aliapa kuheshimu na kutetea Katiba, kutekeleza kwa uaminifu majukumu ya juu aliyokabidhiwa na taifa, na kujitolea juhudi zake zote kuhimiza manufaa ya wote, amani na umoja wa kitaifa.
Pia ameahidi kulinda ukamilifu wa ardhi ya nchi na kujiendesha wakati wote kama mtumishi mwaminifu na mwenye heshima kwa watu.
Chini ya Katiba ya Benin, rais wa jamhuri ana mamlaka ya utendaji na, kama mkuu wa serikali, huamua na kuendesha sera za taifa wakati huohuo huku akitumia mamlaka ya udhibiti. Rais husimamia utawala na vikosi vya jeshi na anawajibika kwa ulinzi wa taifa.
Kufuatia kushauriana na Bunge, rais huteua wajumbe wa serikali, hufafanua majukumu yao na anaweza kuwafukuza kazi.
Wadagni, mwenye umri wa miaka 49, hapo awali alifanya kazi Deloitte kabla ya kuingia serikalini baada ya kuchaguliwa kwa Patrice Talon mwaka 2016. Tangu wakati huo amefanya kazi kama waziri wa uchumi na fedha, aliteuliwa tena mwaka 2021, na baadaye akapandishwa cheo hadi kuwa waziri mkuu, akichukua jukumu muhimu katika kutekeleza sera za kiuchumi za Talon.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma




