Shughuli ya kitamaduni yazidisha mabadilishano ya kati ya watu na watu ya China na Tanzania

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Mei 27, 2026
Shughuli ya kitamaduni yazidisha mabadilishano ya kati ya watu na watu ya China na Tanzania
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa, na Michezo wa Tanzania Paul Makonda akitoa hotuba kwenye saluni ya kitamaduni iliyofanyika Dar es Salaam, Tanzania, Mei 24, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)

DAR ES SALAAM - Saluni ya kitamaduni iliyofanyika Jumapili jioni jijini Dar es Salaam, Tanzania iliwaleta pamoja wasanii kutoka China na Tanzania na kuonyesha dhahiri ubadilishanaji wa kistaarabu unaolenga kuzidisha uhusiano wa kitamaduni kati ya nchi hizo mbili.

Shughuli hiyo, iliyoandaliwa na Ubalozi wa China nchini Tanzania, Kituo cha China cha Ubadilishanaji wa Kimataifa wa Kitamaduni na Kuhimiza Utalii nchini Tanzania, iliwaleta pamoja maafisa wa serikali, wasomi, wasanii, na wajumbe wa jumuiya ya Wachina nchini Tanzania.

Kwa saa zaidi ya mbili, washiriki walizama katika safari ya kitamaduni iliyoandaliwa vema ikijumuisha densi ya jadi ya Kichina, sherehe za chai, maonyesho ya kauri, uonyeshaji wa kutengeneza ubani, na kujaribu na kujionea aina mbalimbali shirikishi za kitamaduni.

Balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian amesema shughuli hiyo ililenga kufufua kumbukumbu za Njia ya Kale ya Hariri ya Baharini, ambayo kihistoria iliunganisha China na Afrika kupitia biashara na mabadilishano ya kitamaduni.

"Njia ya Kale ya Hariri ya Baharini ilitumika kama njia ya kale ya baharini kwa ajili ya mabadilishano ya kiuchumi na kitamaduni kati ya China na sehemu zingine za dunia," Chen amesema, akibainisha kuwa "kwa muda mrefu imekuwa ikitumika kama kifungo cha bluu kinachounganisha ustaarabu wa China na Afrika."

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa, na Michezo wa Tanzania, Paul Makonda ameuelezea utamaduni kuwa ni daraja lenye nguvu ambalo linaimarisha urafiki na kuishi pamoja kwa amani miongoni mwa mataifa.

"Kupitia muziki, densi, utamaduni wa chai, kauri, na vielelezo vingine vya kitamaduni, tunaendelea kuthamini uzuri wa uanuwai na umuhimu wa kuishi pamoja kwa amani," Makonda amesema katika hotuba yake.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha