Cape Verde yaishikilia Hispania kwa sare ya bila kufungana huku mechi zote za usiku wa Jumatatu zikimalizika kwa sare

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Juni 16, 2026
Cape Verde yaishikilia Hispania kwa sare ya bila kufungana huku mechi zote za usiku wa Jumatatu zikimalizika kwa sare
Ferran Torres (kushoto) wa Hispania akishindana kwenye mechi ya kundi H kati ya Hispania na Cape Verde katika Kombe la Dunia la FIFA 2026 katika Uwanja wa Atlanta, Atlanta, Marekani, Juni 15, 2026. (Xinhua/Wang Kaiyan)

ATLANTA, Marekani - Hispania imeanza kampeni yake ya Kombe la Dunia kwa mwanzo wa kukatisha tamaa, kwani imeshikiliwa sare ya 0-0 na Cape Verde katika mechi ya ufunguzi kwa Kundi H ya Kombe la Dunia la FIFA 2026 iliyochezwa Atlanta, Marekani usiku wa kuamkia leo Jumanne huku mechi zingine zote zilizofuata zikikamilika bila kutoa washindi.

Katika mechi hiyo, Hispania ilitawala sehemu kubwa ya mchezo, lakini kipa mkongwe wa Cabo Verde, Vozinha, alifanya kazi mfululizo za kuokoa mpira ili kuweka matokeo sawa.

Katika mechi hiyo ya kwanza kabisa kwa Cape Verde kushiriki katika hatua hiyo na ya kwanza pia kucheza na Hispania katika ngazi ya kimataifa, Hispania ilihangaika kuivunja safu ya ulinzi ya Cape Verde licha ya kufurahia umiliki mzuri.

Mechi inayofuata ya Hispania itacheza na Saudi Arabia, huku Cabo Verde ikicheza na Uruguay.

Katika mechi nyingine, Misri imeilazimisha Ubelgiji sare ya 1-1 katika mchezo wao wa ufunguzi kwa Kundi G ya Kombe la Dunia la FIFA.

Wakicheza dhidi ya moja ya timu ambazo kwa kawaida ni zenye nguvu ya soka barani Ulaya, Misri walichukua uongozi dakika ya 19 wakati kiungo Emam Ashour alipopiga shuti golini baada ya kupewa pasi na nahodha Mohamed Salah kwa bao lake hilo la kwanza kwa timu ya taifa ya wakubwa.

Ubelgiji walisawazisha dakika ya 66 baada ya shinikizo kutoka kwa mchezaji aliyeingia kutoka benchi Romelu Lukaku kumlazimisha beki wa Misri Mohamed Hany kuugeuza mpira kuelekea kwenye nyavu za goli lake mwenyewe.

Mechi nyingine ya Kundi H, imeshuhudia Saudi Arabia ikiishikilia Uruguay katika sare ya 1-1 na kufanya timu za Asia kuendelea kutofungwa hadi sasa kwenye Kombe la Dunia la FIFA 2026.

Wasaudi walipata uongozi wa kushtukiza dakika ya 41. Hassan Altambakti alipiga mpira kwa kichwa kuelekea langoni kutoka kwenye kona. Kipa wa Uruguay Fernando Muslera hakuweza kudhibiti mpira huku Abdulelah Alamri akiupiga kuelekea golini.

Uruguay ilikuwa na nguvu zaidi katika kipindi cha pili lakini haikufanikiwa kupata bao hadi Maximilliano Araujo alipopiga mpira uliokuwa ukirudishwa na upande wa Saudi Arabia na kumpita kipa Mohammed Alowais kutoka karibu na goli dakika ya 80.

Mechi ya mwisho kwa usiku wa kuamkia leo Jumanne, ilikuwa ya Kundi G kati ya New Zealand na Iran ambapo mechi hiyo kama ilivyo kwa mechi zingine za leo imemalizika kwa sare ya 2-2.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha