Lugha Nyingine
Walimu 15 wa Tanzania washinda mashindano ya mafunzo ya kidijitali yanayoungwa mkono na China

Balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian akihutubia hafla ya utoaji wa tuzo ya mashindano ya mafunzo ya kidijitali yanayoungwa mkono na China kwa walimu wa Tanzania katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Tanzania, Agosti 28, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)
DAR ES SALAAM - Waelimishaji 15 bora wa Tanzania wamejitokeza kuwa washindi miongoni mwa washiriki zaidi ya 200 katika mashindano ya mafunzo ya kidijitali yanayoungwa mkono na China, ambayo yamefikia tamati kwa hafla ya utoaji wa tuzo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) siku ya Ijumaa.
Tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo mwishoni mwa mwezi Aprili, mashindano hayo yanayoandaliwa kwa pamoja na Kituo cha Kikanda cha China-Afrika kwa Ushirikiano wa Elimu ya Kidijitali cha Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang, China, UDSM, na Taasisi ya Umoja wa Mfumo wa Mawasiliano ya Vyuo Vikuu vya China-Afrika, limetathmini maingizo kupitia miundo ya ufundishaji na video zinazoonyesha matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika ufundishaji.
Walimu wapatao 222 wa shule za msingi, sekondari na elimu ya juu kutoka mikoa 22 kote Tanzania walishiriki kwenye raundi ya awali, huku walimu 90 wakisonga mbele kwenye raundi ya fainali.
Zaidi ya siku mbili za mashindano ya ana kwa ana, washiriki wa fainali walitathminiwa kupitia uwasilishaji wa somo, vipindi vya mafunzo kwa kuigiza hali halisi ya utoaji mafunzo, na mijadala ya maswali na majibu. Baada ya tathmini ya kina, walimu 15 bora wamechaguliwa.
Huang Xiao, kaimu mkurugenzi wa Kituo cha Kikanda cha China-Afrika kwa Ushirikiano wa Elimu ya Kidijitali cha Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang, amesema mashindano hayo yaliweka mkazo kwenye matumizi ya teknolojia za kidijitali katika mafunzo darasani na kuanzisha mfano wa aina mpya kwa ajili ya kuongeza uwezo wa kidijitali wa walimu kupitia uzoefu wa mafunzo darasani kwa kutegemea teknolojia.
Balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian amesema teknolojia ya kidijitali inabadilisha elimu, sekta mbalimbali na jamii, na kufanya ujuzi wa kidijitali kuwa muhimu zaidi kwa walimu na wanafunzi. Ameongeza kuwa China itaendelea kuunga mkono maendeleo ya elimu ya Tanzania na kuhimiza ushirikiano wa kina zaidi katika elimu ya kidijitali, sayansi na teknolojia.

Walimu wa Tanzania wakishiriki kwenye raundi ya fainali na hafla ya utoaji wa tuzo ya mashindano ya mafunzo ya kidijitali yanayoungwa mkono na China iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Tanzania, Agosti 28, 2026. (Xinhua/Emmanuel Herman)
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



