UN: Watu karibu milioni 25 wanakabiliwa na hali kali ya ukosefu wa usalama wa chakula nchini DRC

(CRI Online) Novemba 13, 2025

Msemaji wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bw. Stephane Dujarric amesema watu karibu milioni 25, asilimia zaidi ya 20 ya watu wote nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), wanakabiliwa na viwango vikubwa vya hali kali ya ukosefu wa usalama wa chakula.

Bw. Dujarric amesema DRC bado ni moja ya nchi zilizoathiriwa zaidi na hali ya ukosefu wa usalama wa chakula, huku hali ikiwa mbaya zaidi katika maeneo ya mashariki mwa nchi hiyo.

Kwa mujibu wa uchambuzi wa hivi karibuni kuhusu usalama wa chakula, idadi ya watu wanaokabiliwa na tatizo hilo inakadiriwa kuongezeka hadi karibu milioni 27 katika nusu ya kwanza ya mwaka 2026.

Dujarric ameongeza kuwa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) bado ina wasiwasi mkubwa kuhusu mashambulizi yanayoendelea dhidi ya raia katika maeneo ya Beni na Lubero katika Jimbo la Kivu Kaskazini na pia katika jimbo la Ituri, huku watu zaidi ya 1,000 wakiripotiwa kuuawa katika majimbo hayo mawili tangu mwanzoni mwa mwaka huu.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Renato Lu)

Picha