Tanzania Yanyakua Tuzo za Juu za Kimataifa za Utalii

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Januari 07, 2026

DAR ES SALAAM, Jan. 6 — Tanzania imepokea tuzo tatu za kimataifa za utalii siku ya Jumatatu, ikionesha hadhi inayozidi kuongezeka ya nchi hiyo ya kuwa moja ya maeneo yanayoongoza kwa utalii unaotegemea mazingira ya asili.

Taarifa kutoka Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais wa Tanzania imesema kuwa tuzo hizo zimewasilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii wa nchi hiyo, Ashatu Kijaji, katika hafla iliyofanyika Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar. Miongoni mwa tuzo hizo ni ile ya hadhi ya Nchi Inayoongoza Duniani kwa Utalii wa Mbugani Mwaka 2025 (World’s Leading Safari Destination 2025).

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Tanzania imenyakua tuzo hiyo katika Fainali Kuu za Tuzo za Utalii Duniani Mwaka 2025 (World Travel Awards 2025) iliyofanyika Desemba 6 nchini Bahrain, ikizishinda nchi nyingine zenye vivutio vya utalii zikiwemo Botswana, Kenya, Namibia na Afrika Kusini.

Aidha, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti imetajwa kuwa Hifadhi ya Taifa Inayoongoza Duniani Mwaka 2025 (World’s Leading National Park 2025), ikizishinda hifadhi maarufu kama vile Hifadhi ya Taifa ya Kruger ya Afrika Kusini na Hifadhi ya Taifa ya Yellowstone ya Marekani.

Visiwa vya Zanzibar vya Tanzania vimeongeza idadi ya tuzo hizo kwa kutajwa kuwa Kituo Bora cha Mapumziko kwa Mashirika ya Kibiashara Barani Afrika Mwaka 2025 (Africa’s Best Corporate Retreat Destination 2025), ikionyesha umuhimu unaozidi kuongezeka wa nchi hiyo katika vyote utalii wa mapumziko na wa biashara.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), idadi ya watalii walioingia nchini humo mwaka 2025 iliongezeka kwa asilimia 9.02 na kufikia milioni 2.09, wakati huohuo mapato yatokanayo na utalii yalifikia rekodi mpya ya dola za Marekani bilioni 4.2.

(Wahariri wa tovuti:Liu Mengxue,Zhao Jian)

Picha