Lugha Nyingine
Tanzania yatangaza kwa umma mkakati wa kitaifa wa elimu ya kidijitali
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya Tanzania Jumatano ilitangaza kwa umma mkakati wa kitaifa wa kuharakisha matumizi ya teknolojia za kidijitali katika ngazi zote za elimu.
Akizungumza kwenye warsha ya wadau wa elimu jijini Dar es Salaam, katibu mkuu katika wizara hiyo, Carolyne Nombo, amesema serikali inapanua elimu ya kidijitali kutoka shule za awali hadi vyuo vikuu, pamoja na taasisi za elimu na mafunzo ya ufundi stadi (TVET).
Amesema mabadiliko ya kidijitali yamekuwa jambo la lazima, kama ilivyoainishwa katika Dira ya Maendeleo ya Tanzania ya 2050, akibainisha kuwa maendeleo ya baadaye ya nchi hiyo yanategemea nguvu kazi yenye ujuzi wa kidijitali.
Amesema utekelezaji wa mkakati huo utaanza kwa kuimarisha miundombinu ya kidijitali, ikiwa ni pamoja na muunganisho wa intaneti, upatikanaji wa vifaa vya kidijitali, na umeme wa kuaminika katika shule, vyuo vya mafunzo ya ualimu, taasisi za TVET, na vyuo vikuu.
Pia amevitaka vyuo vikuu na taasisi za utafiti kuhimiza uvumbuzi katika elimu inayowezeshwa na akili mnemba (AI) ili kuboresha upatikanaji wa mazingira bora ya kujifunza.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



