Lugha Nyingine
Nchi za Ulaya zaungana mkono kupinga ushuru wa Marekani unaolenga Greenland

Bendera ya Umoja wa Ulaya ikionekana mbele ya makao makuu ya Kamisheni ya Ulaya mjini Brussels, Ubelgiji, Julai 7, 2020. (Xinhua/Zhang Cheng)
BRUSSELS – Mpasuko wa uhusiano kati ya pande mbili za Atlantiki kuhusu Greenland umeongezeka kwa kiasi kikubwa jana Jumapili baada ya Ulaya kutoa kwa nadra upingaji wa pamoja dhidi ya vitisho vya ushuru wa adhabu kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump.
Katika mwitikio mkali zaidi wa pamoja hadi sasa, nchi nane zilizolengwa moja kwa moja na ushuru huo uliopendekezwa -- Denmark, Finland, Ufaransa, Ujerumani, Uholanzi, Norway, Sweden, na Uingereza -- zimetoa taarifa ya pamoja zikielezea "mshikamano kamili" na Denmark na Greenland.
Nchi hizo zimeonya kwamba hatua hiyo ya Marekani ina hatari ya kusababisha "mwelekeo hatari wa kushuka" katika uhusiano kati ya pande mbili za Atlantiki na kuahidi kutoa mwitikio "wa pamoja na ulioratibiwa" ili kulinda mamlaka ya nchi.
Rais wa Baraza la Ulaya Antonio Costa amesema kupitia ujumbe kwenye mtandao wa X kwamba Umoja wa Ulaya (EU) uko "tayari kujilinda dhidi ya aina yoyote ya shinikizo la kulazimisha" kufuatia vitisho vya ushuru vya Trump.
Mwitikio wa kitaifa ulikuwa wa haraka na usio na utata, huku viongozi na mawaziri wa Ulaya wakilaani tishio hilo la Marekani wakilielezea kuwa la kulazimisha na lisilokubalika.

Waziri Mkuu wa Denmark Mette Frederiksen akihudhuria mkutano maalum wa viongozi wa Umoja wa Ulaya (EU) mjini Brussels, Ubelgiji, Machi 6, 2025. (Xinhua/Peng Ziyang)
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uholanzi David van Weel ameutaja wazi ushuru huo kuwa ni kitendo cha "shinikizo la kulazimisha," akiitaka Washington kuondoa "pendekezo la kipuuzi" kabla halijaanza kutekelezwa.
Makamu Chansela na Waziri wa Fedha wa Ujerumani Lars Klingbeil amesema Berlin "haitapaswi kujiruhusu kutishwa," akiongeza kwamba "mstari umevukwa."
Waziri Mkuu wa Denmark Mette Frederiksen ameandika ujumbe kwenye mitandao ya kijamii kwamba "Ulaya haitalazimishwa kwa vitishio." Akisisitiza uungaji mkono mpana kwa Denmark, amesema hilo sasa ni "suala linalovuka mipaka ya kitaifa."

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron (kulia) akisalimiana na Waziri Mkuu wa Denmark Mette Frederiksen alipowasili kuhudhuria mkutano wa "Muungano wa Walio tayari" kwenye Ikulu ya Elysee jijini Paris, Ufaransa, Septemba 4, 2025. (Xinhua/Gao Jing)
Ikiuelezea ushuru huo kuwa "haukubaliki," ofisi ya Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron pia imethibitisha kwamba rais huyo ataomba kuchukuliwa kwa hatua kama hiyo endapo Washington itatekeleza tishio lake.
Siku ya Jumamosi, Waziri Mkuu wa Uingereza Minister Keir Starmer alisema msimamo wa Uingereza kuhusu Greenland uko wazi kabisa: "ni sehemu ya Ufalme wa Denmark, na mustakabali wake ni suala la Watu wa Greenland na Denmark," akilielezea tishio la Marekani kuwa "lisilo sahihi kabisa."

Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer (kushoto) akisalimiana na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron kabla ya mkutano wa viongozi wa Uingereza, Ufaransa, Ujerumani na Ukraine katika Mtaa No. 10 wa Downing jijini London, Uingereza, Desemba 8, 2025. (Xinhua/Li Ying)

Waandamanaji wakikusanyika kupinga vitendo vya Marekani na kauli za Marekani zinazodokeza kudhibiti Greenland mjini Copenhagen, Denmark, Januari 17, 2026. (Xinhua/Zhang Yuliang)
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



