Tanzania yatahadharisha kuhusu usumbufu wa usafiri kabla ya msimu wa mvua

(CRI Online) Februari 25, 2026

Wizara ya Uchukuzi ya Tanzania Jumanne ilitoa tahadhari kuhusu usumbufu unaoweza kutokea kwenye huduma za usafiri wa barabara, reli, anga na maji wakati wa msimu wa mvua wa Machi hadi Mei 2026, ikirejelea utabiri wa kunyesha kwa mvua za juu ya wastani.

Katika taarifa yake, wizara hiyo imesema utabiri wa msimu huu wa mvua unaonesha kuwa maeneo ya pwani ya kaskazini, ikiwa ni pamoja na Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Pwani, Dar es Salaam, na visiwa vya Unguja na Pemba visiwani Zanzibar, vilevile sehemu za Bonde la Ziwa Victoria, yanatarajiwa kupata mvua ya wastani hadi juu ya wastani.

Aidha, utabiri huo pia unaonesha kuongezeka kwa mvua kubwa mwezi Aprili, huku kukiwa na uwezekano mkubwa wa matukio mabaya ya hali ya hewa.

Wizara hiyo imebainisha kuwa hali hiyo ya hewa inaweza kuharibu miundombinu ya barabara na reli, kuongeza hatari za ajali za barabarani, na kusababisha ucheleweshaji au kufutwa kwa safari za ndege na huduma za baharini.

Wizara hiyo imewasihi wadau wa usafiri, wakiwemo waendeshaji na mameneja, kuchukua hatua za tahadhari kama vile kufuatilia utabiri wa kila siku wa hali ya hewa, kuzingatia miongozo ya usalama, na kuimarisha ukaguzi wa miundombinu ili kupunguza uharibifu unaoweza kutokea kutokana na mafuriko.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha