Muungano wa Shea Duniani yafungua mkutano wake wa 2026 nchini Ghana kwa kujikita katika uongezaji thamani (3)

(Tovuti ya Gazeti la Umma) April 29, 2026
Muungano wa Shea Duniani yafungua mkutano wake wa 2026 nchini Ghana kwa kujikita katika uongezaji thamani
Mwonyeshaji akionesha tunda la shea katika mkutano wa Shea 2026, Accra, Ghana, Aprili 28, 2026. (Picha na Seth/Xinhua)

ACCRA – Muungano wa Shea Duniani, The Global Shea Alliance (GSA), inayojumuisha wadau wa tasnia ya uzalishaji na biashara ya kokwa za shea, siagi ya shea, na bidhaa nyingine za shea, umefungua mkutano wake wa mwaka wa "Shea 2026" mjini Accra, mji mkuu wa Ghana, kwa kujikita katika uongezaji thamani ili kupata manufaa makubwa zaidi ya kiuchumi kutoka kwa bidhaa za shea.

Makamu Rais wa Ghana Jane Naana Opoku-Agyemang amesema kwenye ufunguzi wa mkutano huo kwamba nchi za Afrika zinatarajiwa kupata manufaa bora ya kiuchumi, kwa kubadilika kutoka kuuza nje kokwa ghafi za shea hadi kuuza nje bidhaa za shea zilizoongezwa thamani.

Opoku-Agyemang amesisitiza kwamba kuna mamia ya maelfu ya wanawake wa Ghana, hasa katika sehemu za kaskazini mwa nchi hiyo, wanaojihusisha na shughuli za shea, ambapo miti ya shea ni sehemu ya maisha ya kila siku, ikitoa chakula na mapato na kutoa mchango katika mauzo ya nje.

Ametoa wito kwa nchi nyingine za Afrika zinazozalisha shea kubuni na kutekeleza sera ambazo zitazifanya nchi zao kuwa wauzaji nje wa bidhaa za shea zilizokamilika na zilizokamilika nusu badala ya kuuza nje kokwa ghafi.

John Owan Enoh, waziri wa nchi anayeshughulikia viwanda katika Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ya Nigeria, amesema kwamba Nigeria imeshuhudia ongezeko kubwa la usindikaji wa shea wa ndani tangu serikali ilipoweka zuio la kuuza nje kokwa ghafi.

Enoh amesema maendeleo hayo yamesababisha kuimarika tena kwa bei za mazao katika ngazi ya shamba, upanuzi wa uwezo wa viwanda, ukuaji wa uwekezaji katika uuzaji nje wa bidhaa za shea zilizosindikwa, na kuongezeka kwa shauku kutoka kwa wanunuzi wa kimataifa katika ushirikiano wa usindikaji wa ndani.

GSA iliyoanzishwa mwaka 2011, inabuni, kuendeleza, na kutekeleza mikakati inayochechea tasnia ya shea yenye ushindani na uendelevu duniani kote ili kuboresha maisha ya wanawake wa vijijini barani Afrika na jamii zao zinazotegemea tasnia hiyo, na hivyo kuchangia afya ya mfumo wa ikolojia kwa ujumla na kuhakikisha kwamba manufaa ya tasnia hiyo ya shea yanatambuliwa na kugawiwa miongoni mwa wadau wote.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha