Lugha Nyingine
Waziri Mkuu wa Uingereza Starmer atangaza kujiuzulu

Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer akitoa hotuba nje ya Mtaa No. 10 wa Downing jijini London, Uingereza, Juni 22, 2026. (Xinhua)
LONDON - Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer ametangaza katika hotuba nje ya Mtaa No. 10 wa Downing jijini London jana Jumatatu kwamba atajiuzulu nafasi ya kiongozi wa Chama tawala cha Labour na kuweka ratiba ya kuondoka kwake ofisini.
Starmer amesema amesikia jibu la wabunge wa Labour kwa swali la kama alikuwa na nafasi nzuri ya kukiongoza chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao.
"Ninakubali jibu hilo kwa neema," amesema.
Starmer amesema atabaki ofisini kama waziri mkuu hadi uchaguzi wa uongozi wa Labour utakapokamilika na "kufanya kila niwezalo kuhakikisha makabidhiano ya madaraka kwa utaratibu."
Ameongeza kuwa atampa mrithi wake "uungaji mkono wake kamili na usio na shaka."
Starmer amesema ataiomba Kamati Tendaji ya Kitaifa ya Labour kupanga ratiba, ambapo uteuzi wa wagombea utafunguliwa Julai 9 na kufungwa kabla ya mapumziko ya majira ya joto ya Bunge. Kama mgombea zaidi ya mmoja ataingia kwenye kinyang'anyiro hicho, uchaguzi wa uongozi utakamilika kwa wakati ambapo kiongozi mpya atakuwa tayari amepatikana kabla ya Bunge kurejea mwezi Septemba.
Starmer alianza rasmi kuwa waziri mkuu mwezi Julai 2024 baada ya kukiongoza chama cha Labour kushinda katika uchaguzi mkuu, na kumaliza miaka 14 ya utawala wa chama cha Conservative.
Akifanya kampeni chini ya kauli mbiu ya "mabadiliko," Starmer aliahidi kufufua ukuaji uchumi, kuboresha huduma za umma, kupunguza uhamiaji usiofuata utaratibu na kurejesha utulivu baada ya miaka mingi ya misukosuko ya kisiasa nchini Uingereza.
Nafasi yake hiyo imekuwa chini ya shinikizo linaloongezeka huku kukiwa na ukosoaji wa sera za uhamiaji na nishati za serikali, utata unaoendelea kumzunguka balozi wa zamani wa Uingereza nchini Marekani Peter Mandelson juu ya uhusiano wake na Jeffrey Epstein, na wito unaoongezeka kutoka ndani ya chama cha Labour kwa Starmer kujiuzulu.
Andy Burnham, ambaye wakati huo alikuwa meya wa Greater Manchester, alishinda uchaguzi mdogo wa ubunge wa jimbo la Makerfield Juni 19 na kurudi katika Baraza la Wawakilishi, jambo ambalo linaonekana sana kuwa kichocheo cha kujiuzulu kwa Starmer.
Baada ya Starmer kutangaza kujiuzulu kwake, Burnham amethibitisha kwamba ataingia katika kinyang'anyiro cha kumrithi. "Nitajitokeza mwenyewe mbele kuwa sehemu ya mchakato huu," amesema.
Kiongozi wa Chama cha Conservative Kemi Badenoch amejibu kwa kuchapisha tena taarifa hiyo ya Burnham kwenye mtandao wa X na kuandika: "Kama hautagombea, tunasubiri nini?"
Kiongozi wa chama cha Reform UK Nigel Farage amedai uchaguzi mkuu siku hiyo. Akiandika kwenye mtandao wa X, Farage amesema Reform UK "inadai uchaguzi" na iko "tayari kuleta mabadiliko makubwa."

Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer na mkewe wakitembea kutoka nje ya Mtaa No. 10 wa Downing jijini London, Uingereza, Juni 22, 2026. (Xinhua)

Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer akimkumbatia mkewe jijini London, Uingereza, Juni 22, 2026. (Xinhua)
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



