Mkoa wa Hunan Katikati mwa China waongeza biashara kati ya China na Afrika kwa uvumbuzi wa sera

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Juni 23, 2026

Watu wakitembelea banda la Afrika Kusini kwenye Kituo cha Kimataifa cha Maonyesho na Mikutano cha Changsha mjini Changsha, Mkoa wa Hunan, katikati mwa China, Juni 12, 2025. (Xinhua/Wang Jingqiang)

Watu wakitembelea banda la Afrika Kusini kwenye Kituo cha Kimataifa cha Maonyesho na Mikutano cha Changsha mjini Changsha, Mkoa wa Hunan, katikati mwa China, Juni 12, 2025. (Xinhua/Wang Jingqiang)

CHANGSHA – Kwenye soko lenye pilika nyingi mjini Changsha, mji mkuu wa Mkoa wa Hunan, katikati mwa China, wanunuzi wanachagua bidhaa maalum za Afrika. Mteja mmoja anajaribu sampuli ya losheni ya mwili iliyotengenezwa kwa siagi ya shea kutoka Mali, ambayo ina umbo la krimu nyeupe na harufu tamu.

"Shukrani kwa sera ya China ya kutotoza ushuru, gharama za malighafi ziko chini zaidi kwa asilimia 20 hadi 25, na tunapitisha faida hizo moja kwa moja kwa watumiaji," amesema Zuo Dongnan, ambaye amekuwa akifanya biashara kati ya China na Mali kwa muda mrefu.

"Kwa sasa tunaagiza tani takriban 300,000 za malighafi kila mwaka na kiasi chetu cha uagizaji kitaendelea kukua." Ameongeza.

Pia katika mji huo wa Changsha, ukumbi wa maonyesho wa kudumu katika Soko Kuu la Gaoqiao unaonyesha bidhaa kutoka nchi zote 53 za Afrika ambazo zina uhusiano wa kidiplomasia na China. Ukumbi huo pia una vituo vya huduma, zikiwemo ofisi ya mawasiliano kati ya taasisi za biashara za China na Afrika, ikitoa huduma ya ulinganishaji wa wanunuzi na wauzaji mwaka mzima.

Ingawa haina bandari, Hunan imeibuka kuwa mwanzilishi wa ushirikiano wa kiuchumi kati ya China na Afrika kupitia uvumbuzi wa sera.

Ikiwa ni mwenyeji wa kudumu wa Maonyesho ya Kiuchumi na Biashara ya China na Afrika (CAETE), mkoa huo umewezesha miradi 512 iliyosainiwa yenye thamani ya dola bilioni 64.71 za Marekani katika maonyesho ya awamu nne zilizopita. Biashara yake na Afrika imedumisha yuan zaidi ya bilioni 50 (dola za Marekani karibu bilioni 7.34) kwa miaka mingi mfululizo.

Zaidi ya maonyesho hayo ya kila baada ya miaka miwili mjini Changsha, waandaaji wamepeleka tukio hilo nje ya nchi hadi Kenya, Morocco na mataifa mengine ya Afrika, wakichunguza mahitaji ya ndani ya mashine za kilimo, magari ya nishati mpya na vipuri vya magari ili kuhakikisha ulinganishaji mahsusi wa kibiashara.

Kampuni nyingi katika Eneo la Biashara Huria la Majaribio la China (Hunan) pia zimeanzisha ubia na washirika wa Nigeria, zikitoa huduma jumuishi zikiwemo za usafiri, maghala, usambazaji, usindikaji, ufungashaji, usimamizi wa marejesho na ufadhili wa biashara.

Tangu Mei, China imepanua sera yake ya ushuru-sifuri hadi kuhusisha nchi zote 53 za Afrika ambazo zina uhusiano wa kidiplomasia nayo. Hata hivyo, biashara ya kimataifa ya bidhaa za kilimo inakabiliwa na mahitaji ya ukaguzi na karantini. Ili kurahisisha zaidi kuingia kwa bidhaa za kilimo za Afrika, Hunan ilizindua mifumo ya mwanzo kabisa ya tathmini ya awali ya vyakula vya Afrika vinavyosafirishwa kuuzwa China.

Mfumo huo unaruhusu wataalamu wa China kupitia viwango vya uzalishaji na usindikaji kabla ya bidhaa kusafirishwa, hali ambayo inafupisha kwa kiasi kikubwa vipindi vya ukaguzi.

Matokeo ni dhahiri. Mwaka 2025, uagizaji bidhaa nje wa Hunan kutoka Afrika ulikua kwa asilimia 27.2 hadi yuan bilioni 30.92. Watumiaji wa China sasa wanafurahia mananasi freshi ya Benin, maharagwe ya kahawa ya Ethiopia na maharagwe ya kakao ya Uganda, wakati huohuo uagizaji wa karanga za makadamia za Afrika Kusini na parachichi za Kenya unatarajiwa kupanuka zaidi.

Lauren Johnston, profesa msaidizi katika Kituo cha Stadi za China cha Chuo Kikuu cha Sydney, hivi karibuni alisifu uvumbuzi wa kisera wa Hunan, akiuita "Njia ya Hunan" kwa nguvu bora zake za kuzidisha na kuleta uwiano mkubwa zaidi katika biashara kati ya China na Afrika na ufungamanishaji wa viwanda, na kuisaidia Afrika kushinda vizuizi vikuu vya maendeleo.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha