Lugha Nyingine
Naibu Waziri ya Mambo ya Nje wa Iran atangaza kukamilika kwa mazungumzo ya Doha juu ya utekelezaji wa makubaliano ya Iran-Marekani

Picha hii iliyopigwa Juni 30, 2026 ikionyesha mandhari ya maghorofa katika wilaya ya West Bay, Doha, Qatar. (Picha na Nikku/Xinhua)
TEHRAN - Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayeshughulikia Masuala ya Kisheria na Kimataifa Kazem Gharibabadi ametangaza kukamilika kwa mazungumzo nchini Qatar jana Jumatano juu ya utekelezaji wa makubaliano ya amani (MoU) kati ya Iran na Marekani.
Akiongoza ujumbe kutoka Wizara ya Mambo ya Nje, Benki Kuu, na Wizara ya Kilimo, Gharibabadi amesema kwamba timu ya Iran imefanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Qatar ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje Sheikh Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim Al Thani asubuhi na kisha kuhudhuria mikutano miwili na wajumbe wa Qatar na Pakistan, kwa mujibu wa shirika rasmi la habari la Iran, IRNA.
"Mkutano wa kwanza wa kundi la usimamizi wa utekelezaji wa MoU pia umefanyika kwa ushiriki wa wapatanishi waandamizi kutoka nchi hizo tatu," amesema.
Kwa mujibu wa shirika hilo la habari, kwenye majadiliano hayo, ujumbe wa Iran umebainisha na kujadili ukiukaji wa Marekani wa wajibu wake chini ya Kifungu cha 1 cha MoU, kinachohusu kumalizwa kwa vita nchini Lebanon, habari za hatua za Marekani kuhusu uimarishaji wa vifaa na vikosi vyake vya kijeshi katika eneo la Asia Magharibi, na kauli za "vitisho na uingiliaji kati" kutoka kwa maafisa wa Marekani.
Gharibabadi amesema ujumbe wa Iran umesisitiza kwamba majukumu ya pande husika chini ya MoU ni seti jumuishi na hayapaswi kutazamwa kwa kutengana, na kuongeza kwamba imeamuliwa kwamba njia ya mawasiliano ya dharura ya kundi la ufuatiliaji itaanzishwa ifikapo leo Alhamisi na ukiukwaji wa MoU utaripotiwa, kujadiliwa, na kuamuliwa kwa njia rasmi na iliyowekwa katika maandishi.
Amebainisha kuwa katika mikutano na maafisa wa Qatar, wakiwemo wawakilishi wa benki kuu, masuala maalum yanayohusiana na matumizi ya sehemu ya mali zilizozuiliwa za Iran zenye thamani ya dola bilioni 6 za Marekani yalijadiliwa, na imeamuliwa kwamba, kulingana na mahitaji ya Iran, bidhaa muhimu zitanunuliwa na kupewa nchi hiyo.
Gharibabadi amesisitiza kwamba hakuna mkutano wa moja kwa moja uliofanyika kati ya wajumbe wa Iran na Marekani mjini Doha.
Kwa mujibu wa IRNA, sambamba na mikutano hiyo ya timu ya Iran mjini Doha, ujumbe wa Marekani, unaoongozwa na mjumbe maalum wa Rais Donald Trump wa Marekani Steve Witkoff na mkwewe Jared Kushner, pia ulikuwa nchini Qatar na umefanya mikutano na maafisa wa Qatar.

Jamaa akiwa amesimama ndani ya jengo la tawi la benki lililoharibiwa wakati wa machafuko ya hivi karibuni mjini Tehran, Iran, Januari 21, 2026. (Xinhua/Shadati)
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma



