Lugha Nyingine
Indaba ya Uzalishaji Bidhaa yaangazia uwekezaji, mafungamano ya kikanda kwa maendeleo ya viwanda ya Afrika (4)
![]() |
| Watu wakizungumza kwenye maonyesho ya Indaba ya Uzalishaji Bidhaa 2026 (2026 Manufacturing Indaba) mjini Johannesburg, Afrika Kusini, Julai 14, 2026. (Xinhua/Chen Wei) |
JOHANNESBURG - Maafisa wa serikali, wazalishaji, na wawekezaji wametoa wito wa uwekezaji imara zaidi, mafungamano ya kina zaidi ya kikanda, na ushirikiano wa karibu wa sekta ya umma na binafsi ili kuharakisha maendeleo ya viwanda ya Afrika kwenye maonyesho ya Indaba ya Uzalishaji Bidhaa 2026 (2026 Manufacturing Indaba) mjini Johannesburg, Afrika Kusini.
Akihutubia shughuli hiyo ya siku mbili kuanzia Jumanne, Naibu Waziri wa Biashara, Viwanda, na Ushindani wa Afrika Kusini John Steenhuisen amesema uzalishaji bidhaa ni msingi wa maendeleo ya viwanda, akibainisha kuwa kuijenga upya sekta hiyo ni muhimu katika kutengeneza ajira, kuongeza mauzo ya nje, na kuchochea ukuaji wa muda mrefu wa uchumi.
"Uzalishaji bidhaa unabaki kuwa uti wa mgongo wa kila uchumi wa viwanda uliofanikiwa. Una uwezekano mkubwa wa kutengeneza ajira endelevu, kuchochea uvumbuzi wa kiteknolojia, kuongeza tija, kuchochea mauzo ya nje, na kuzalisha mahitaji katika uchumi mzima," amesema.
Naibu waziri huyo ameongeza kuwa Afrika Kusini itafuata mkakati wa viwanda unaojikita katika sekta mbalimbali za uchumi, kuondoa gesi chafuzi, na kuingiza mambo ya kidijitali ili kurudisha nyuma hali ya kudorora kwa viwanda, kuimarisha uzalishaji bidhaa wa ndani, na kuboresha uwezo wa ushindani wa nchi hiyo.
Vuyiswa Ramokgopa, mjumbe wa Baraza Kuu la Kilimo na Maendeleo Vijijini katika Jimbo la Gauteng nchini Afrika Kusini, amesema kujenga mazingira ya biashara rafiki kwa wawekezaji na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi itakuwa muhimu katika kufungua nguvu bora za viwanda za Afrika.
"Serikali haziwezi kulifanya bara kuwa na maendeleo ya viwanda peke yake," amesema, akiongeza kuwa ushirikiano wa karibu miongoni mwa serikali za Afrika, wawekezaji, na wazalishaji utasaidia kufungua fursa mpya chini ya Eneo la Biashara Huria la Bara la Afrika (AfCFTA) kwa kuhimiza uwekezaji mkubwa wa ndani ya Afrika, ushirikiano wa viwanda, na uzalishaji wa kuvuka mipaka.
Waonyeshaji bidhaa kwenye mkutano wa mwaka wa shughuli hiyo wamesema shauku ya wawekezaji katika sekta ya uzalishaji bidhaa ya Afrika inaendelea kuongezeka, hasa katika uzalishaji wa magari, usindikaji wa mazao ya kilimo, nishati mbadala, dawa, na teknolojia za hali ya juu za uzalishaji bidhaa.
Carlos Manuel, mwonyeshaji bidhaa wa Msumbiji anayewakilisha kampuni ya masuluhisho ya uzalishaji bidhaa, amesema AfCFTA inahimiza kampuni kupanuka zaidi ya masoko ya ndani kupitia ushirikiano wa kikanda.
“Kwa kuchangia utaalamu na kuwekeza katika uzalishaji wa ndani, kampuni za Afrika zinaweza kuwa na ushindani zaidi na kupunguza utegemezi wa uagizaji,” Manuel amesema, akiongeza kuwa "AfCFTA inafungua fursa mpya kwa wazalishaji kufanya kazi pamoja kuvuka mipaka."
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma




