Misri yashuhudia idadi inayovunja rekodi ya watalii milioni 19 katika mwaka 2025 (2)

(Tovuti ya Gazeti la Umma) Januari 05, 2026
Misri yashuhudia idadi inayovunja rekodi ya watalii milioni 19 katika mwaka 2025
Picha hii iliyopigwa Januari 1, 2026 ikionyesha watalii wakitembelea Piramidi za Giza nchini Misri. (Xinhua/Ahmed Gomaa)

CAIRO - Misri ilipokea idadi inayovunja rekodi ya watalii karibu milioni 19 mwaka 2025, ambayo imefikia ongezeko la asilimia 21 ikilinganishwa na mwaka 2024 , Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale wa Misri Sherif Fathy amesema.

Fathy amesema ongezeko hilo limetokana na hali ya usalama na utulivu, mkakati bayana wa maendeleo, pamoja na juhudi za kuzifanya bidhaa za utalii kuwa za aina mbalimbali na kuboreshwa kwa huduma.

“Cairo, Hurghada, Sharm El-Sheikh, na Marsa Alam vilikuwa viwanja vya ndege vyenye pilika nyingi vya nchi, ikionyesha kusambaa kijiografia kwa vivutio vya utalii vya Misri,” alisema siku ya Jumamosi, akiongeza kuwa ndege za watalii zimefika Cairo kutoka miji 193 duniani kote.

Amesema, idadi ya ndege maalum za kukodi iliongezeka kwa asilimia 32 mwaka 2025, huku Mji Mpya wa Alamein ukijitokeza kuwa eneo linalokua kwa kasi la shughuli za utalii, ambapo ndege za kukodi zimefikia ongezeko la asilimia 450.

Shughuli za Utalii ni chanzo kikuu cha fedha za kigeni kwa Misri, pamoja na pesa zinazotumwa na Wamisri wanaoishi ng'ambo, mapato ya Mfereji wa Suez na mauzo ya nje. Sekta hiyo imeendelea kuimarika baada ya kuzalisha dola bilioni 15.3 za Marekani mwaka 2024 kutoka kwa watalii milioni 15.7.

(Wahariri wa tovuti:Song Ge,Zhao Jian)

Picha