Mkurugenzi Mkuu wa ILO asema mivutano ya kibiashara duniani imeathiri soko la ajira

(CRI Online) Juni 03, 2025

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Gilbert Houngbo, amesema mvutano wa sasa wa biashara ya kimataifa umeongezeka, ukiathiri soko la ajira katika nchi mbalimbali.

Akihutubia Mkutano wa 113 wa Kimataifa wa Kazi ulioanza jana Jumatatu mjini Geneva, Uswisi, Bw. Houngbo amesema kwa mujibu wa Ripoti ya ILO kuhusu makadirio ya ajira na jamii duniani, idadi ya ajira mpya duniani inatarajiwa kuwa milioni 53 mwaka huu, ikiwa ni pungufu kwa milioni 7 kutoka milioni 60 iliyotarajiwa Oktoba mwaka jana.

Ameeleza kuwa, sababu kuu ya mabadiliko hayo ni kuongezeka kwa mivutano ya kibiashara ambayo imesababisha kudorora kwa ukuaji wa uchumi duniani.

Bw. Houngbo pia amesema matumizi ya akili mnemba (AI) yanazidi kuwa na athari kubwa kwenye soko la ajira la kimataifa.

(Wahariri wa tovuti:Zhou Linjia,Zhao Jian)

Picha