

Lugha Nyingine
Ukraine, Russia zapata maendeleo katika mazungumzo ya amani ya Istanbul, zakubaliana mabadilishano makubwa ya wafungwa
![]() |
Waziri wa Ulinzi wa Ukraine Rustem Umerov (katikati) akizungumza na waandishi wa habari mjini Istanbul, Uturuki, Juni 2, 2025. (Xinhua/Liu Lei) |
ISTANBUL - Wajumbe wa Ukraine na Russia wamepata maendeleo katika mazungumzo mapya ya amani mjini Istanbul siku ya Jumatatu, ikiongeza matumaini madogo juu ya uwezekano wa kupunguza uhasama kupitia hatua zilizopanuliwa za kibinadamu, ikiwemo mabadilishano makubwa ya wafungwa tangu kuanza kwa mgogoro huo.
Mkutano huo wa takribani dakika 90 umeashiria duru ya pili ya mazungumzo ya moja kwa moja kati ya pande hizo mbili katika wiki za hivi karibuni ambapo maafisa wa Uturuki wameelezea matokeo hayo kuwa "ya matumaini mwangalifu."
"Mazungumzo hayakuisha vibaya," msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki Oncu Keceli amesema, akielezea hali ya mazungumzo hayo kuwa ya kiujenzi licha ya kuwa na tofauti juu ya mgogoro mpana zaidi.
Makubaliano juu ya hatua za kibinadamu
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan, ambaye ameongoza mazungumzo hayo, ameandika katika ujumbe wake kwenye mtandao wa kijamii wa X kwamba wajumbe hao wameegemea kwenye mambo yaliyokubaliwa hapo awali, ikiwa ni pamoja na hatua zinazohusiana na mabadilishano ya kibinadamu.
"Kuna makubaliano juu ya vipengele vipya na kuongezeka kwa idadi ya wafungwa watakaobadilishwa," Fidan ameandika.
Waziri wa Ulinzi wa Ukraine, Rustem Umerov, akiongoza ujumbe wa Kiev, amependekeza usimamishaji vita bila masharti kwa siku 30, kurejeshwa kwa watoto waliokimbia makazi yao na askari vijana, na kuachiliwa kwa wafungwa.
Umerov ametoa wito wa "juhudi za kweli za kumaliza vita," na amependekeza kufanyika kwa duru ya tatu ya mazungumzo kati ya Juni 20 na 30, kama sehemu ya juhudi mpana zaidi za kuelekea mkutano unaowezekana wa viongozi.
Ujumbe wa Russia, ukiongozwa na Msaidizi wa Rais Vladimir Medinsky, umethibitisha makubaliano juu ya kile alichokielezea kuwa ni mabadilishano makubwa zaidi ya wafungwa tangu mgogoro huo uanze.
"Askari wote waliojeruhiwa vibaya na wagonjwa mahututi watabadilishwa, pamoja na wanajeshi wote waliokamatwa chini ya umri wa miaka 25," amesema.
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma